![]() |
| Uchangiaji Damu Salama kusaidia wagonjwa wenye uhitaji wa damu imeelezwa na Chama cha Wasanii wa filamu na picha jongefu wa mkoa wa Geita (TDFAA) kwamba sasa ni jambo la muhimu wala sio hiari tena. |
Na Urban Epimark, GEITA
Suala la kuchangia damu salama kuokoa maisha ya wagonjwa hospitalini na wanaopata ajali limeelezwa sasa kuwa ni la muhimu kwa jamii na sio tena jambo la hiari.
Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa chama cha wasanii wa filamu na picha jongevu wa mkoa wa Geita (TDFAA) Bi Rosemary Michael kwenye maonesho yanayoendelea mjini Geita ya teknolojia ya madini na uwekezaji.
"Uhitaji wa damu ili kusaidia wagonjwa hospitalini pamoja na akina mama wanaojifungua na wanao pata ajali kwa sasa ni mkubwa hivyo si jambo la hiari tena bali ni la muhimu" alieleza Mwenyekiti wa wasanii.
Bi Rosemary Michael aliongeza kwa kusema wasanii kama sehemu ya jamii jukumu lao kubwa ni kutoa elimu kwa njia ya kuhamasisha jamii kujua jukumu hilo kwa kupitia kazi zao za usanii.
Hata hivyo, Mwenyekiti huyo aliongeza kwa kusema kwamba, wasanii tunao wajibu wa kuchangia pia damu ili kuokoa maisha ya wengine waliopo hospitalini na kwingineko.
Halikadhalika ameishukuru kampuni ya GF Trucks & Equipments ya mjini Kibaha mkoa wa Pwani kwa kufadhili wasanii hao kuweza kuchangia damu pamoja na gharama zingine kuwezesha majukumu yao.
Nae Mratibu wa huduma ya damu salama katika mkoa wa Geita Bw Charlse Mateso amewashukuru wasanii hao kwa moyo wao wa kizalendo wa kuchangia damu.
Bw Mateso alibainisha zaidi kwamba, uhitaji wa damu kwa mkoa wa Geita ni wastani wa chupa 450 kwa mwezi ambapo mahitaji makubwa yapo kwa akina mama wanao jifungua pamoja na watoto chini ya miaka 5.
Kituo hicho cha benki ya damu salama cha Halmashauri ya Mji wa Geita kilijiwekea lengo la kupata chupa 210 za damu kwa muda wa siku katika maonesho haya ya madini lakini kwa muda wa siku 5 tangu maonesho yaanze Sept 27, 2022 tayari wameshapata jumla ya chupa 153 sawa na asilimia 73 ya lengo.
Mwisho.




0 Comments