TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

TARURA GEITA YAZIDI KUPAA: MWENGE WA UHURU WAWEKA JIWE LA MSINGI BARABARA YA KASCO


Na Victor Bariety, Geita

Septemba 2, 2025


Picha: Mkimbiza Mwenge Kitaifa  2025 akimpongeza Mkuu wa Wilaya ya Geita, muda mfupi  baada ya kuweka jiwe la msingi mradi wa barabara ya Kasco.

Kilio cha wananchi wa Geita kuhusu changamoto za miundombinu kinaendelea kupata majibu ya vitendo. Leo, katika eneo la Kasco hadi Shule ya Sekondari Nyanza, Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025 umeweka jiwe la msingi kwenye mradi wa ujenzi wa barabara ya lami nyepesi yenye urefu wa kilomita 1.32, hatua inayoongeza chachu ya maendeleo kwa wakazi wa Manispaa ya Geita.

 

Picha: Mkimbiza Mwenge Kitaifa  2025 akisoma maandishi kwenye jiwe la msingi mradi wa barabara ya Kasco

Mradi huo unaotekelezwa na Halmashauri ya Manispaa ya Geita kupitia fedha za mapato ya ndani, unasimamiwa na TARURA Geita huku mkandarasi akiwa ni kampuni ya Evax Construction Ltd ya Mureba. Kwa mujibu wa mkataba namba 63CC1/2924/2025/W/03, gharama ya ujenzi ni shilingi 999,950,000.00 bila VAT.


Kwa mujibu wa taarifa ya Meneja wa TARURA Wilaya ya Geita, Injinia Bahati Subeya, mradi huo ulianza Machi 7, 2025 na unatarajiwa kukamilika Septemba 8, 2025. Hadi sasa umefikia asilimia 95 ya utekelezaji, ambapo zaidi ya shilingi milioni 754 zimeshalipwa.

Picha: Meneja TARURA Wilaya ya Geita  akisoma taarifa ya mradi.

Akisoma taarifa kwa niaba ya Halmashauri na wananchi wa Kalangalala, Injinia Subeya alisema mradi huo utakuwa na manufaa makubwa kwa wananchi, yakiwemo kupunguza adha ya usafiri wakati wote wa mwaka, kuchochea biashara na kuboresha mandhari ya mji.

 


Baada ya kukagua mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ndg. Ismail Ali Ussi, alisifu ubora wa utekelezaji akisema hakuna chembe ya ubabaishaji.

 “Nimetembea mikoa 24, huu ni mkoa wa 25. Sikuwahi kuona miradi ya kiwango cha juu kama hii inayotekelezwa na TARURA. Jana nilizindua barabara ya Nzera, leo Kasco, yote kwa ubora wa hali ya juu. Hakuna harufu ya ufisadi, hakuna ubabaishaji – kazi hii inastahili saluti,” amesema Ussi huku akishangiliwa na wananchi.

 


Aliongeza kuwa miradi inayotekelezwa chini ya usimamizi wa TARURA ni ushahidi kuwa kodi zinazotozwa kwa wananchi zinatendewa haki. Pia aliipongeza Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Geita kwa kuendelea kulinda amani, jambo lililompa faraja kubwa katika ziara hiyo ya kitaifa.

 


Kabla ya kuweka jiwe la msingi, Ndg. Ussi alitumia nafasi hiyo kuwasihi wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 kwa amani na utulivu, akisisitiza kuwa miradi mikubwa inayotekelezwa kote nchini ni matunda ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.

 “Kura zetu ndizo zinazoamua hatima ya maisha yetu. Uchaguzi ni msingi wa amani na maendeleo tunayoyaona. Rais wetu Samia amethibitisha kwa vitendo – miradi hii ni uthibitisho. Oktoba tumpe kura nyingi ili aendelee kutupigania,” amesisitiza kiongozi huyo wa mbio za Mwenge.

 


Barabara ya Kasco ni ya pili kutembelewa na Mwenge wa Uhuru ndani ya Manispaa ya Geita baada ya jana kuzinduliwa barabara ya Nzera Center yenye urefu wa kilomita 1.1, ambayo pia ilipewa sifa kwa kiwango cha juu cha ubora.

 


Picha: Barabara iliyowekewa jiwe na msingi

Kwa hatua hizi, Geita inaendelea kuandika historia ya mafanikio makubwa ya miradi ya TARURA, miradi inayobadilisha uso wa miji na vijiji, huku wananchi wakiona matunda ya kodi zao kwa macho.

 

Picha: Akikagua mradi

Imeandaliwa na Victor Bariety – 0757 856 284

PICHA ZAIDI



Picha: Akikagua mradi

Picha: Hamasa 


 Picha: Ukaguzi wa mradi unaendelea

 Picha: Kulia Meneja wa TARURA mkoa akiwa na mgombea Ubunge Jimbo la Geita Chacha Wambura Mwita 




Post a Comment

0 Comments