TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

MWENGE WA UHURU WAZINDUA BARABARA YA NZERA CENTER KWA GHARAMA YA ZAIDI YA SHILINGI MILIONI 737


Na Victor Bariety, Geita

 

Leo katika Kata ya Nzera, Wilaya ya Geita, Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025 umefanya uzinduzi rasmi wa mradi wa ujenzi wa barabara ya Nzera Center yenye urefu wa kilomita 1.1 kwa kiwango cha lami nyepesi.


Picha: Barabara iliyozinduliwa

Katika risala ya mradi huo, iliyosomwa na Meneja wa TARURA Wilaya ya Geita, Injinia Bahati Subeya, ilielezwa kuwa barabara hiyo imetekelezwa kwa awamu mbili. Awamu ya kwanza ilianza tarehe 24 Julai 2023 na kukamilika tarehe 15 Oktoba 2024 kwa gharama ya shilingi 499,995,000/=. Awamu ya pili ilianza tarehe 22 Machi 2024 na kukamilika tarehe 15 Oktoba 2024 kwa gharama ya shilingi 237,499,984/=. Hivyo kufanya jumla ya mradi kufikia thamani ya shilingi 737,494,984/=.

Picha: Barabara iliyozinduliwa

Aidha, hadi sasa mkandarasi amelipwa kiasi cha shilingi 714,270,224/=, ikiwa ni malipo ya kazi zote zilizokamilika. Mradi huu umesimamiwa na TARURA Wilaya ya Geita na umefikia asilimia 100 ya utekelezaji. Faida zake zimeanza kuonekana wazi kwa wananchi, ikiwemo kurahisisha usafiri na usambazaji wa huduma za kijamii, kuchochea maendeleo ya kiuchumi, na kuboresha mandhari ya eneo husika.


Picha: Wafanyakazi TARURA wakiwa kwenye picha ya pamoja  kwenye jiwe la msingi muda mfupimara baada ya mradi huo kuzinduliwa

Akizungumza kabla ya kuzindua mradi huo, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025, Ndg. Ismail Ali Ussi, alitoa pongezi za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha fedha za umma zinatumika ipasavyo. Alisema hakuamini kuona mradi wa kiwango cha juu namna hiyo ukiwa na thamani ndogo ukilinganisha na matokeo yaliyopatikana.

 “Ndugu zangu, sikutegemea Nzera ningeweza kukuta mradi mzuri kama huu. Fedha iliyotumika ni ndogo lakini matokeo ni makubwa. Hakuna ubabaishaji, TARURA mmemtendea haki Rais wetu. Hongereni sana kwa mradi huu,” amesema Ndg. Ussi huku akishangiliwa na wananchi.


Picha: Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru akisoma maandishi yaliyopo kwenye jiwe la msingi muda mfupi baada ya kuzindua mradi huo

Aidha, kiongozi huyo wa Mwenge alisisitiza umuhimu wa wananchi kushiriki kwa amani na utulivu katika Uchaguzi Mkuu wa 2025, akieleza kuwa miradi kama hii ni matunda ya Serikali inayojali wananchi wake bila kujali itikadi za vyama. Alisisitiza kuwa barabara hii ni ya kudumu na itaendelea kuhudumia wananchi kwa miaka mingi ijayo, hivyo ni jukumu la kila mmoja kuitunza.

Akiongea na mwandishi wa habari hizi kwa niaba ya wananchi wake, Mbunge wa Jimbo la Geita Vijijini anayemaliza muda wake na ambaye amefanikiwa kutetea kiti hicho, Mhe. Joseph Kasheku Musukuma, alisema kazi zinazotekelezwa na Serikali ya CCM chini ya Rais Samia Suluhu Hassan ni kubwa na zimekuwa chachu ya wananchi kuendelea kuiamini serikali yao.

 “Hata mimi kutetea kiti hiki nimebebwa na utekelezaji wa miradi mikubwa na ya kimkakati katika jimbo langu. Wananchi wameona na wanaguswa moja kwa moja na matokeo yake. Ndiyo maana ninawaomba Oktoba mwaka huu kura zijae kwa mgombea urais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, wabunge na madiwani wa CCM kuanzia jimboni kwangu hadi nchi nzima. Kuchagua upinzani ni sawa na kurudisha nyuma maendeleo tuliyoyapata,” amesema Mhe. Musukuma.

 

Wananchi wa Nzera waliokuwa wamejitokeza kwa wingi kushuhudia tukio hilo walipokea pongezi hizo kwa makofi na vigelegele, wakionyesha furaha yao kwa namna mradi huo umebadili sura ya kata yao na kuwa chachu ya maendeleo endelevu. 

PICHA ZAIDI



Picha:Kiongozi wa mbio za mwenge wa uhuru kitaifa akiongea na wananchi kabla ya uzinduzi wa mradi huo.
Picha: Meneja Tarura Wilaya ya Geita akisoma risala kwa mkimbiza mwenge kitaifa.






Post a Comment

0 Comments