TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

TABIBU AHUKUMIWA KWENDA JELA MIAKA MITATU KWA KOSA LA KUOMBA NA KUPOKEA RUSHWA YA SHILINGI ELFU 30 WILAYANI GEITA

 


Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita imemhukumu Afisa Tabibu wa kituo cha Afya cha Katoro wilayani Geita kwa makosa ya  kuomba na kupokea Rushwa ya shilingi Elfu 30 kinyume na kifungu cha 15 cha Sheria Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11/2007 .

 Aliyehukumiwa kwenda jela baada ya kutiwa hatiani na mahakama  ni Samson Lameck Kuzenza aliyekuwa Afisa Tabibu  kituo cha Afya katoro katika kesi Namba  402/2019 iliyokuwa ikisikilzwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Geita.

 Akisoma hukumu hiyo  Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu mkazi Geita, Mheshimiwa . Obadia Bwegoge alisema Mshtakiwa amepatikana na hatia katika makosa yote mawili ya Kuomba na Kupokea Rushwa kinyume na kifungu cha 15 cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na. 11/2007 na kwamba atatumikia kifungo cha miaka mitatu jela kwa kila kosa.

 Mheshimiwa Hakimu Obadia Bwegoge alifafanua kuwa  ushahidi uliowasilishwa na upande wa Jamhuri ukiongozwa na Wakili wa TAKUKURU Augustino Mtaki  umethibitisha pasipo kuacha shaka kwamba Mshtakiwa Samson Lameck Kuzenza akiwa Afisa Tabibu  alitenda kosa hilo  mnamo tarehe 07 Desemba 2019 akiwa katika Kituo cha Afya cha Katoro.

 Mheshimiwa  Bwegoge alibainisha  kwamba kwa mjibu wa ushahidi, Mtuhumiwa baada ya kuomba fedha hizo hakumhudumia mgonjwa mpaka alipozidiwa ndipo alipomhudumia kwa masharti kwamba asingemruhusu kutoka kituoni hapo mpaka atoe fedha hizo na kwamba huduma ya mama wajawazito hutolewa bure hivyo utozaji wa fedha hizo ni Rushwa na kwa kuzingatia  ushahidi wa  wa pande zote mbili akaamuru  mshtakiwa kwenda jela miaka mitatu kwa kila kosa na kutupilia  mbali utetezi wake wa kuomba kuonewa huruma . 

Awali mwendesha mashtaka wa TAKUKURU Augustino Mtaki akiuongoza upande wa jamhuri aliiambia Mahakama  kuwa Mshtakiwa   Samson Lameck Kuzenza ambaye alikana  mashtaka kuhusika baada ya kuosomewa mahakamani hapo  anadaiwa kutenda kosa hilo  Desemba 7 mwaka 2019 kwa muomba Rushwa ya Shilingi 30,000/=  Bwana Said Kulwa Msuluzya ili amfanyie usafi mke wake ambaye ni Bi.Sheha Hashim Hussein aliyepata tatizo la kuharibikiwa mimba. 

Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Geita  Leonidas Felix kwa njia ya simu ametumia fursa hiyo kutoa wito kwa watumishi wa umma na wananchi katika kukemea vitendo vya kuomba na kupokea rushwa.

Post a Comment

0 Comments