TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

MGODI UMELIPONGEZA GAZETI LA RAIA MWEMA KWA KUANDIKA HABARI ZILIZOZAA MATUNDA

Katibu wa Mgodi wa Isanjabadugu,Patrick Basoga akifafanua jambo baada ya mgodi wake kupata Leseni.

Na Paul Kayanda, Mbogwe

UONGOZI wa Mgodi wa Isanjabadugu unaomilikiwa na kikundi cha Wachimbaji wadogo Kata ya Nyakafulu Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe Mkoani Geita umelipongeza Gazeti la Raia Mwema kwa kuandika Habari za kilio cha ukosefu wa Leseni jambo ambalo limezaa matunda.

Gaezeti la Raia Mwema limekuwa likiandika mara kadhaa Habari za Mgodi huo kuomba Leseni ili kuondokana na Usimamizi wa Mfumuko wa Madini (RUSH) na kuwa Mgodi kamili unaotambulika kwa mujibu wa sheria sheria za Madini ili kuwekeza zaidi na kuongeza pato la Serikali.

Mgodi huo umesema kuwa umetambua nguvu ya vyombo vya Habari ambavyo pia vimeripoti mara kwa mara kuunga juhudi za Mgodi kuiambia serikali ione umuhimu wa kutoa leseni kwa mgodi huo ambao unamilikiwa na wachimbaji wadogo kinachojulikana kwa jina la ISANJABADUGU na kwamba sasa wamepata leseni ili kuwekeza zaidi na hatimaye uwe mgodi wa Uchimbaji wa kati.

Makamu mwenyekiti wa mgodi wa Isanjabadugu Sang'udi Mpigahodi akizungumza na mtandao huu juu ya namna watakavyoboresha shughuli za uchimbaji wa Madini ya Dhahabu baada ya kupewa leseni na serikali.

Kaimu Mwenyekiti wa Mgodi huo Sang’udi Hamis Mpigahodi alisema hayo jana alipokuwa akiongea na Waandishi wa Habari Ofisini kwake na kwamba anavishukuru vyombo vya Habari hususani Gazeti la Raia Mwema pamoja na Bodi ya Isanjabadugu vilivyo saidia kuikumbusha serikali kwa kuandika Habari juu ya hitaji la Leseni kwani shughuli hizo ziliendeshwa kwa hofu ya kuondolewa wakati wowote.

Pia Mgodi wa Isanjabadugu unaishukuru serikali chini ya Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na tume ya madini inayoongozwa na Waziri wa Madini Dkt.Doto Biteko kwa kusikia kilio cha wachimbaji wadogo  na kuwapatia Leseni hiyo kwani ni vikundi vingi vya matajiri vilikuwa vinalihitaji eneo hilo.

Mpiga hodi alieleza kuwa Mgodi huo uliendeshwa kwa kipindi cha miaka mitano bila kuwa na leseni walitumia mfumo wa Rush huku wakikusanya maduhuli ya serikali jambo ambalo limepelekea baadhi ya wawekezaji wenye mitaji mikubwa kushindwa kuwekeza kwa hofu ya kufukuzwa kutokana na mgodi huo siyo rasmi.

Makamu mwenyekiti huyo wa Mgodi Mpiga Hodi alisema kuwa kitendo cha serikali kuwapatia leseni hiyo wachimbaji wadogo kwenye eneo la Nyakafuru ahadi yao ni kuongeza juhudi ya uchimbaji na uzalishaji na kuhakikisha kuwa serikali itapata mapato zaidi ya yale waliyopata kipindi mgodi siyo rasmi.

Mama,Rais wetu tunashukuru sana kwa kusikia kilio chetu cha miaka mingi kwa kweli tunashukuru kutoka kwenye sakafu ya mioyo yetu, Nisemetu sasa tumepata leseni kwa maana mgodi sasa ni rasmi sisi tumejipanga kuchimba na kuongeza pato la serikali, na wawekezaji wataongezeka mwanzo watu waliogopa kuwekeza mitaji yao mikubwa kwa hofu ya kubaki ndege kwenye eneo hili,” alisema Mpigahodi makamu mwenyekiti wa mgodi.

Naye Meneja wa Mgodi huo Modesta Wisero alisema kuwa baada ya kupata leseni hiyo anatoa ahadi ya kusimamia vyema maduhuli ya serikali yataongezeka mara mbili ya kile walichokuwa wakizalisha wakati mgodi haukuwa rasmi na kuongeza kuwa hiyo ni kwa sababu wanakwenda kuwekeza mahali ambapo ni sahihi.

Hata hivyo katibu wa Mgodi huo Patrick Basoga pamoja na wachimbaji wengine kwa pamoja wanasema kuwa kwa sasa tatizo na changamoto iliyopo kwa sasa ambayo inapelekea kupungua kwa maduhuli ya serikali ni kukatika hovyo kwa umeme, uzalishaji wa Mgodi wake kwa miezi miwiwili iliyopita unashuka kwa kuchangiwa na hilo.

“Kama Mgodi tunaomba mamlaka inayohusika na Nishati ya umeme ijitahidi kulekebisha ama kutatua changamoto hii ili umeme ujeree kama kawaida maana hata ukiwaka huwa hauna nguvu ya kusukuma mashine zetu za uchimbaji, leo sisi kama mgodi tumepewa Leseni tutachimba madini ya Dhahabu kwa amani bila hofu ya kufukuzwa na kama umeme utakuwa kama awali uzalishaji utaongezeka mara dufu.

Athman Ipangalala ni mchimbaji aliyewekeza kwenye mgodi huo anasema kuwa kama wawekezaji wamechimba kwa kipindi kirefu bila leseni kwa maana mguu moja ndani na mwingine nje huku wakiogopa kuweka nguvu nyingi kwa hofu ya kula hasara.

Mwekezaji huo anasema lakini kwa sasa anaishukuru serikali ya Rais Samia kwa kuona na kusikia kilio chao kupitia vyombo vya Habari na hatimaye wamepatiwa leseni na sasa uwekezaji wao utakuwa na tija na kuahidi kutokwepa mapato ya serikali ama utoroshaji.

Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Mkoani Geita Said Nkumba akiteta jambo namwandishi wa Habari juu ya Upatikanaji wa Leseni hiyo.

Akizungumzia hatua hiyo wakati akizungumza na gazeti hili ofisini kwake, Mkuu wa Wilaya ya Bukombe ambaye anakaimu ofisi ya mkuu wa Wilaya ya Mbogwe, Saidi Nkumba anasema kimsingi anamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutoa maelekezo kwenye sekta ya Madini lakini Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko ametekeleza majukumu yake vyema kwenye sekta hiyo.

Aliongeza kuwa Mgodi wa Isanja badugu kabla ya kupata leseni walipochimba madini hayo kupitia mfumo wa RUSH walifanya mambo makubwa mengi ikiwemo kutekeleza miradi mikubwa mingi kwenye jamii na vijiji vinavyozunguka Mgodi wao, na waliweza kukusanya mapato ya serikali kupitia mirabaha mbalimbali na kuongeza kuwa mwezi Octoba walikabidhiwa Leseni jambo ambalo litawapa moyo wa kufanya shughuli za Uchimbaji kwa weredi ukilinganisha ni miaka mingi wanaisotea.

Hayo ni maelekezo ambayo Rais amekuwa akiyatoa mara kwa mara ili kuhakikisha kwamba Wachimbaji wadogo nchini wananufaika na rasrimali zao zilizopo kwenye maeneo yao na nchi kwa ujumla  na nimatumaini yangu kwamba kwa maelekezo hayo Wachimbaji kwenye sekta ya Madini watanufaika kwa namna moja ama nyingine,” alisema Said Nkumba Mkuu wa Wilaya ya Bukombe.

Wachimbaji wadogo na mafundi matimba wakionesha furaha yao baada ya mgodi wao kupewa Leseni.

Mwisho.

Post a Comment

0 Comments