TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

VITUO VYA CHUO KIKUU HURIA TANZANIA KUUNGANISHWA NA MKONGO WA TAIFA

Mgeni Rasmi katika Mahafali ya 41 ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) ambae ni Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Philip Mpango akiongea na wahitimu hao katika viwanja vya Furahisha jijini Mwanza leo November 24, 2022.

Na Urban Epimark, MWANZA

Serikali imeagiza vituo vyote vya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania hapa nchini viunganishwe na Mkongo wa Taifa ili kupunguza gharama za uendeshaji huku wahitimu wa chuo hicho wameaswa kutumia vema elimu wanayopata  kuleta tija kwa Taifa.

Hayo yamesemwa Jijini Mwanza na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Phillip Mpango wakati wa mahafali ya 41 ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) ambapo alikuwa Mgeni Rasmi.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Philip Mpango akiwa katika Mahafali ya 41 ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania jijini Mwanza yaliyofanyika viwanja vya Furahisha leo November 24, 2022

Aidha, Mhe. Mpango ameagiza Wizara ya Elimu kuhakikisha  mpango huo unafanyika haraka wa kuviinaunganishaa vituo hivyp na mkongo wa Taifa haraka ili kuwezesha matumizi ya TEHAMA na kupunguza mzigo wa gharama kwa wanavyuo pamoja na uendeshaji kwa upande wa uongozi.

"Vituo vyote vya Chuo Kikuu Huria  viunganishwe na mkongo wa Taifa na  hili naagiza Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kuhakikisha linafanyika haraka ili kusaidia kupunguza gharama za uendeshaji," ameongeza Mhe. Dkt Mpango. 

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt Philip Mpango (katikati) akiwa kwenye parade la ukakamavu pamoja na Waziri Mkuu Mstaafu wa Serikali ya Awamu ya Nne ya Tanzania Mhe Mizengo Peter Pinda (kushoto) na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Adolf Mkenda (kulia) pamoja na viongozi wengine katika viwanja vya Furahisha jijini Mwanza leo November 24, 2022

Awali akiongea katika mahafali hayo, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda, alisema Chuo Kikuu Huria  cha Tanzania (OUT)  kimetengewa fedha kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET) kwa ajili ya  ujenzi wa miundo mbinu pamoja na kusomesha wahadhiri na pia kufanikisha miradi mingine.

Sehemu ya wahitimu wa Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) wakiwa katika Mahafali ya 41 ya Chuo hicho yaliyofanyika viwanja vya Furahisha jijini Mwanza leo November 24, 2022

"Serikali kwa kutambua mchango wa Chuo  Kikuu Huria cha Tanzania katika kupeleka elimu kwa jamii kupitia mradi wa HEET tutajenga maabara saba katika mikoa ya Njombe, Arusha, Dodoma na Mwanza" alisema Waziri Mkenda.

Halikadhalika mikoa mingine itakayo nufaika na fedha hizo ni pamoja na Kigoma, Mtwara na Pwani.

Waziri Mkenda alifafanua zaidi kwamba fedha hizo zitawezesha chuo hicho kujikita zaidi katika tafiti za kisayansi kulingana na shughuli na mahitaji muhimu ya eneo husika.

Wakati huo huo Waziri Mkenda ameongeza kwa kusema kwamba Serikali imetoa zaidi ya Shilingi Bilioni 1.8/= kwa ajili ya kujenga vituo vya Chuo Kikuu Huria cha Yanzania katika mikoa ya Geita, Kigoma, Lindi, Simiyu na Manyara ambapo mikoa hii ilikuwa ikitumia majengo ya kukodi kwa gharama kubwa.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof Adolf Mkenda akitoa hotuba yake kwenye Mahafali ya 41 ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) yaliyofanyika kwenye viwanja vya Furahisha jijini Mwanza leo November 24, 2022

Zaidi ya Wahitimu 4,000 wametunukiwa Shahada mbalimbali za Chuo Kikuu Huria cha Tanzania,  zikiwemo Shahada za Umahiri na Uzamivu wakiwemo pia wanafunzi kutoka nchi jirani za Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi.

Wanafunzi wengine wa kigeni ni kutoka mataifa ya  Ghana, Malawi, Zambia, Congo, Namibia na Ethiopia ambapo nao wametunukiwa Shahada  katika mahafali hayo yaliyofanyika viwanja vya Furahisha jijini Mwanza.

Baadhi ya umati wa watu na wageni mbalimbali walio hudhuria Mahafali ya 41 ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT) yaliyofanyika viwanja vya Furahisha jijini Mwanza wakifuatilia kwa makini matukio katika Mahafali hayo leo November 24, 2022.

Mwisho.

Post a Comment

0 Comments