TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

WALIMU WALIPWE STAHIKI ZAO KWA WAKATI KAMA ILIVYO PANGA SERIKALI.

 

Mkuu wa Wilaya ya Geita Mhe Wilson Shimo ambae alikuwa Mgeni Rasmi katika tukio la kufunga Wiki ya Elimu ya Watu Wazima akimpongeza Mwanafunzi wa Shule ya Msingi Mbugani ya Mahitaji Maalum (mlemavu wa macho) Stephen Joshua baada ya kusoma kwa ufasaha herufi kwa kutumia alama za wasioona wakati Mkuu wa Wilaya alipotembelea maonesho ya shughuli za wadau wa Elimu katika uwanja wa CCM Kalangalala leo November 10, 2022.

Na Urban Epimark, GEITA

Mamlaka zinazo wasimamia na kuwalipa haki zao waalimu wa makundi yote katika wilaya ya Geita wametakiwa kuwalipa waalimu stahiki zao zilivyo  pangwa na serikali kwa wakati ili waweze kuendelea kufundisha kwa moyo.

Mamlaka hizo ni pamoja na watendaji wa Halmashauri ya Mji na Wilaya ya Geita pamoja na Chama cha Waalimu (CWT) na zinginezo zinazo simamia waalimu.

Rai hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya ya Geita Mhe Wilson Shimo kwenye kilele cha kuhitimisha Wiki ya Elimu ya Watu Wazima iliyofanyika Uwanja wa CCM Kalangalala leo November 10, 2022.

"Natoa pongezi nyingi kwa wadau wa elimu katika wilaya yetu ya Geita kuendelea kuthamini mchango wa Wiki ya Elimu  ya Watu Wazima lakini pia nitoe rai kwamba, kile kilichopangwa na serikali kwa ajili ya kuwalipa waalimu mamlaka zifanye hivyo  kwa wakati ili waweze kuendelea kufundisha kwa moyo" alisema.


Mkuu wa Wilaya ya Geita Mhe Wilson Shimo (kushoto mwenye skafu) akisikiliza maelezo kutoka kwa Mwalimu Charles Malima (shati la doti doti) anae fundisha Darasa la 6 & 7 katika Shule ya Msingi Nguzo 2, iliyopo Kata ya Kalangalala, Halmashauri ya Mji wa Geita kuhusu aina mbalimbali za vifaa vya kufundishia kwa njia ya picha na alama ili kukuza zaidi uelewa wa kusoma, kuandika na kuhesabu. Kifaa aina ya "Karikenya" chenye uwezo wa kuchezesha viongo vya mwili wa mwanadamu ndicho kilichomvutia zaidi Mkuu wa Wilaya katika maonesho hayo leo November 10, 2022.

Mkuu wa Wilaya aliendelea kueleza zaidi kwamba, jamii ishirikiane kikamilifu kuhimiza mahudhurio ya wanafunzi shuleni kwa makundi yote lakini pia viongozi, wasimamizi na wadau wote wa elimu waendelee kujitoa kuiboresha sekta ya  elimu ili iweze kuleta tija zaidi kwa Taifa.

Halikadhalika Mkuu wa Wilaya Mhe Wilson Shimo ametoa rai kwa jamii kutumia fursa ya Elimu ya Masafa kujiendeleza kielimu ili kujipatia maarifa mapya ya kukabiliana na changamoto za kimaisha, 

"Ni zamu yetu sisi wananchi bila kujali rika kutumia mpango huu wa elimu ya masafa na mambo mengine yeyote yanayosaidia upatikanaji wa Elimu ambapo hata kama upo njema ya mfumo, itumieni itasaidia" amesisitiza DC Shimo.


Mkuu wa Wilaya ya Geita Mhe Wilson Shimo akikagua kifaa cha kufundishia watoto wa darasa la Awali baada ya kupatiwa maelezo kutoka kwa Mwalimu Florence Walela wa Shule ya Msingi Kalangalala (kulia aliye shika Mike) kwenye maonesho ya zana za kufundishia katika tukio la kufunga Wiki ya Elimu ya Watu Wazima ilitofanyika Uwanja wa CCM Kalangalala leo November 10, 2022

Ameshauri pia kwamba, jamii iendelee kuwafichua wanao waficha walemavu ili wasikose fursa ya kupata elimu kwani Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia imetoa fursa nyingi za kusoma, hata mtu akiwa mtu mzima.

Kuhusu uboreshaji wa mazingira ya kufundishia Mkuu wa Wilaya amesema, mipango ifanyike kuongeza madarasa yanayotumiwa na wanafunzi wa  mfumo wa MUKEJA kwani bado lipo tatizo kwa jamii kujua kusoma, kuandika na kuhesabu (KKK).

Jambo jingine aliloshauri ni kuwezeshwa mifumo ya madarasa ya kufundishia pamoja na waalimu wa Mpango wa Uwiano kati ya Elimu na Jamii, kwa kifupi MUKEJA. 


Kwaya ya Wanafunzi kutoka Shule ya Sekondari ya Geita (GESECO) wakiimba mbele ya Meza Kuu wakati wa kipindi cha kutoa burudani mbalimbali kwenye kilele cha kuhitimisha Wiki ya Elimu ya Watu Wazima katika Halmashauri ya Mji wa Geita iliyofanyika leo November 10, 2022

Nae Afisa Elimu ya Watu Wazima katika Halmashauri ya Mji wa Geita Bi Recho Mwera wakati akisoma taarifa ya utekelezaji ya Elimu ya Watu Wazima alisema, 

"Hali ya utoaji elimu kwa makundi maalum sio ya kuridhisha  sana kwa sababu ya kutokuwezeshwa vyema kwa waalimu na pia baadhi ya wazazi kuendelea kuficha walemavu" alisema Afisa Elimu Watu Wazima. 

Pia alitaja sababu zingine ni pamoja na jamii kuzongwa zaidi na shughuli za kijamii au kimaisha na wengine kukosa uelewa wa elimu ya watu wazima na manufaa yake.


Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Nyankumbu Mwalimu Georgia Mugashe (kulia mwenye kitenge) akiimba na kucheza na kwaya wa wanafunzi kutoka Shule ya Geita Adventists mbele ya Mgeni Rasmi Mkuu wa Wilaya ya Geita Mhe Wilson Shimo kwenye kilele cha kihitimisha Wiki ya Elimu ya Watu Wazima iliyofanyika Uwanja wa CCM Kalangalala leo November 10, 2022.

Wiki ya Elimu ya Watu Wazima hufanyika kila mwaka kote nchini ikiwa lengo lake ni kutoa fursa kwa watu wazima kukutana na kutathmini jinsi ya kuendeleza jamii na kuhamasishana juu ya kuandikasha watoto shule katika umri sahihi.

Kaulimbiu ya mwaka huu ni kuboresha mazingira ya kujifunzia kusoma, kuandika na kuhesabu yatakayozingatia ubora, usawa na utumishi wa makundi yote.


Wanafunzi wa MEMKWA walio rudishwa shuleni baada ya kujifungua wanaosoma Shule ya Sekondari ya Kasamwa iliyopo Halmashauri ya Mji wa Geita wakiimba Shairi la Kumshukuru na Kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa Upendo na Huruma yake kuwarudisha shuleni na kufufua tena upya ndoto za maisha yao kwenye kilele cha kuhitimisha Wiki ya Elimu ya Watu Wazima iliyofanyika Uwanja wa CCM Kalangalala leo November 10, 2022


Wazazi, Walezi, Wanafunzi na washiriki mbalimbali waliohudhuria kilele cha kuhitimisha Wiki ya Elimu ya Watu Wazima iliyofanyika Uwanja wa CCM Kalangalala leo November 10, 2022


Mkuu wa Wilaya ya Geita ambae alikuwa Mgeni Rasmi katika ufungaji Wiki ya Elimu ya Watu Wazima iliyofanyika Uwanja wa CCM Kalangalala akimsalimu Mtoto mwenye Ulemavu wa Ngozi (Albino) anae soma Shule ya Mahitaji Maalum ya Mbugani iliyopo Halmashauri ya Mji wa Geita baada ya wanafunzi hao kuimba wimbo ulio mgusa Mgeni Rasmi leo November 10, 2022

Mwisho.

Post a Comment

0 Comments