TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

HALMASHAURI NCHINI ZATAKIWA KUANDAA MAZINGIRA MAZURI YA UWEKEZAJI

Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt. Grace Magembe akitoa hotuba yake ya kufunga mafunzo elekezi kwa Maafisa Mipango na Sekretarieti za mikoa yaliyofanyika Manispaa ya Morogoro na kufungwa rasmi leo Alhamisi February 02, 2023.


Na Urban Epimark - MOROGORO 

Maafisa Mipango wa Halmashauri pamoja na Sekretarieti za Mikoa Nchini wametakiwa kuandaa mazingira mazuri na wezeshi ya   uwekezaji katika Mamlaka zao za Serikali za Mitaa Nchini.

Rai hiyo imetolewa leo Alhamisi Februari 02, 2023 na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Miko na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt. Grace Magembe kwaniaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI Mhe. Bi. Angellah Kairuki  katika hafla ya kufunga Mafunzo juu ya Uandishi wa Maandiko ya Miradi ya kibiashara ambayo yataziwezesha Halmashauri hapa nchini kufungua Makampuni ya kiuwekezaji kibiashara iliyofanyika kwa siku kumi katika Manispaa ya Morogoro.

Dkt. Magembe amewatata washiriki wa mafunzo hayo  kutumia vyema ujuzi walioupata kwenye mafunzo hayo kuandaa mazingira mazuri na wezeshi yatakayo vutia wawekezaji kutoka sekta binafsi kuwekeza katika Halmashauri zetu na kusema,

“Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anafanya jitihada kubwa za kuifungua nchi yetu kiuwekezaji kwa kujenga mazingira mazuri yanayowavutia wawekezaji kuja kuwekeza katika nchi yetu , hivyo ndugu zangu Maafisa Mipango kupitia ujuzi mlioupata nendeni mkaweke  mazingira wezeshi katika Halmashauri zetu kwa ajili ya wawekezaji wa ndani na nje  kuwekeza katika Halmashauri zenu kwa kufungua Makampuni” alisema Dkt. Magembe.

Washiriki wa mafunzo hayo elekezi ambao ni Maafisa Mipango kutoka ngazi ya Halmashauri na Sekretarieti za mikoa nchini wakimsikiliza Naibu Katibu Mkuu-TAMISEMI Dkt. Grace Magembe (hayupo pichani) alipokuwa akifunga mafunzo hayo mjini Morogoro leo Alhamisi February 02, 2023

Aidha, Dkt. Magembe   amekipongeza Chuo cha Mipango pamoja na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kwa kuandaa  mafunzo hayo yenye tija kwani yamejumuisha nadharia na vitendo kitu kilichowezesha washiriki kuibuka na  maandiko chanya ya kibiashara.

“Naomba niwapongeze na kuwashukuru sana Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini (IRDP) pamoja na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kwa kuandaa na kuendesha vyema mafunzo haya yenye tija ” aliongeza Dkt. Magembe.

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha Mipango ya Maendeleo Vijijini Prof. Hozen Mayaya amesema mafunzo hayo elekezi yaliyofanyika kwa nadharia na vitendo yametoa jumla ya maandiko kumi na tatu (13) ya kibiashara ambayo yataziwezesha Halmashauri kuyawasilisha kwenye taasisi za kifedha kwa ajili ya kupata Mikopo ya kuanzisha Makampuni (SPV).


Mkuu wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) Prof. Hozen Mayaya akitoa salamu za chuo hicho kuishukuru Serikali pamoja na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa- UNDP kwa kuwezesha mafunzo hayo wakati wa ufungaji rasmi mjini Morogoro leo February 02, 2023

Nae Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa  (UNDP)   Bw. Emmanuel Nnko akizungumza kwa njia ya mtandao amekishukuru Chuo cha Mipango kwa utafiti ambao ulibainisha changamoto ya ukosefu wa vyanzo vya uhakika  vya mapato katika Halmashauri nchini na hivyo kuandaa mafunzo haya. 

Vile vile   ameishukuru Serikali kupitia Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa ushirikiano inaotoa kwa taasisi hizi mbili na ameahidi kuendelea kutoa ushirikiano wa kutosha katika kutatua changamoto za maendeleo ikiwemo  kusaidia upatikanaji wa  vyanzo vya mapato katika Halmashauri Nchini. 

Aidha; aimeiomba  Ofisi ya Rais - TAMISEMI   kuipa kipaombele miongozo ya uwekezaji iliyopo katika kila Mkoa.


Mratibu wa Mafunzo hayo ambae ni Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) Dkt. Bonamax Mbassa akieleza jinsi mafunzo hayo yalivyokuwa ya tija kwa washiriki alipopatiwa nafasi ya kusema neno kwa niaba ya washiriki wote wakati wa ufungaji mafunzo hayo mjini Morogoro leo February 02, 2023


Mwisho.

Post a Comment

0 Comments