TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

SERIKALI IMEITAKA JAMII KUJIFUNZA UMUHIMU WA NYUKI NA KUZALISHA ASALI NA MAZAO YAKE KIBIASHARA.

Mgeni Rasmi katika ufunguzi wa maonesho ya Siku ya Nyuki Duniani yanayo fanyika kitaifa mkoani Singida Mkuu wa mkoa huo Mhe Peter Serukamba ambae amewakilishwa na Mkuu wa wilaya ya Singida Mjini Mhandisi Pascal Muragili (kushoto) akiwa na Diwani wa Kata ya Kitaraka iliyopo Halmashauri ya wilaya ya Itigi, wilaya ya Manyoni Mhe John Emanuel (kulia) wakibeba mzinga wa kisasa wa nyuki tayari kwa kuutundika leo Mei 19, 2023 katika msitu wa Kataraka unao simamiwa na Wakala wa Misitu nchini TFS.

Na Urban Epimark, SINGIDA

Serikali imetoa wito kwa jamii nzima ya kitanzania kujifunza na kujua umuhimu na faida za mdudu nyuki ili iweze kumpenda na kumtunza vyema kwa njia ya kisasa kwa faida ya jamii nzima.

Wito huo umetolewa leo Mei 19, 2023 kwenye ufunguzi wa maonesho ya kitaifa ya maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani yaliyo anza jana Mei 18, 2023 na  kuzinduliwa leo Mei 19, 2023 na Mkuu wa mkoa wa Singida Mhe Peter Serukamba ambae amewakilishwa na Mkuu wa wilaya ya Singida Mjini Mhandisi Pascal Muragili. 

"Serikali inapenda kutoa wito kwa jamii nzima kujifunza na kuzielewa faida na umuhimu wa mdudu nyuki katika maisha ya kila siku, ambapo husaidia kuchavusha maua ya mimea mbalimbali ya kuzalisha chakula ambapo ndicho chanzo cha uhai wa viumbe akiwemo binadamu" alisema Mgeni Rasmi.

Akiwa katika ziara ya kutundika mizinga ya kisasa kwenye shamba la msitu wa Kataraka, katika Halmashauri ya wilaya ya Itigi, wilayani Manyoni, Mkuu wa wilaya Mhandisi Pascal Muragili alisema kuanzia mwaka 2017 hadi sasa 2023  serikali imekuwa ikitekeleza mpango mkakati wa ufugaji nyuki kisasa na pamekuwa na maendeleo makubwa.

Mkurugenzi wa Misitu na Nyuki nchini Bw Bivoyo Deusdedit (mwenye miwani) akisoma taarifa ya serikali ya mpango wa ufugaji nyuki kisasa pamoja na uzalishaji wa Asali kibiashara mbele ya Mgeni Rasmi Mkuu wa wilaya ya Singida Mjini Mhandisi Pascal Muragili (hayupo pichani) katika eneo la kijiji cha ufugaji nyuki kata ya Kitaraka, Halmashauri ya wilaya ya Itigi, wilaya ya Manyoni leo Mei 19, 2023

Amezitaja takwimu za vikundi vya ufugaji nyuki kisasa kuwa vimeongezeka  pamoja na pato linalo ingia serikalini kupitia sekta hii na kusema mdudu nyuki ni rafiki na mdau muhimu sana katika maisha ya jamii na kiuchumi kwa ujumla.

Nae Mkurugenzi wa Misitu na Nyuki hapa nchi Bw Bivoyo Deusdedit katika taarifa yake mbele ya Mgeni Rasmi wakati wa utundikaji mizinga ya nyuki ya kisasa katika kata ya Kataraka, Halmashauri ya wilaya ya Itigi, wilaya ya Manyoni amesema, serikali imepania kubadilisha mtindo wa ufugaji nyuki kienyeji na kufanya uwe wa kibiashara.

Meneja mradi wa kuendeleza ufugaji nyuki kisasa wa BEVIC Bw Martin Mgallah, mradi  unaofadhiliwa na Jumuiya ya Ulaya (EU) amesema, mradi umetoa mizinga 500 kwa vikundi 10 vya ufugaji nyuki ambapo kila kikundi kimepatiwa mizinga 50.

Meneja wa Mradi wa BEVAC Bw Martin Mgallah (pichani anae ongea) ambae ni msimamizi wa mradi wa kuendeleza ufugaji nyuki kisasa na kuzalisha Asali kibiashara unao fadhiliwa na Jumuiya ya Ulaya (EU) na kutekelezwa na Enabel katika mikoa ya Singida, Tabora, Shinyanga, Kigoma, Katavi na Pemba akielezea jinsi mradi huo ulivyotoa mizinga 500 ya kisasa kwa vikundi 10 vya ufugaji nyuki mbele ya Mgeni Rasmi Mkuu wa wilaya ya Singida Mjini Mhandisi Pascal Muragili (hayupo pichani) leo Mei 19, 2023 katika msitu wa Kata ya Kataraka, Halmashauri ya wilaya ya Itigi, wilaya ya Manyoni Singida.

Bw Mgallah aliendelea kufafanua kwamba, mradi wa BEVAC unatekelezwa katika mikoa mitano nchini ikiwemo mkoa wa Singida, Tabora, Shinyanga, Katavi na Pemba.. 

Wakati huo huo vikundi vya ufugaji nyuki katika kata ya Kataraka, Halmashauri ya wilaya ya Itigi,  wilaya ya Manyoni imeiomba serikali isaidie kutatua changamoto wanazo kabiliana nazo katika ufugaji nyuki ili waweze kupata tija zaidi.

Kiongozi wa vikundi hivyo vya ufugaji nyuki Bw Meshack Amos alitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na kuongezeka wadudu waharibifu, ukosefu wa vifaa vya urinaji, ukosefu wa mawasikiano ya simu na barabara katika maeneo wanako fugia na ukosefu wa maji.  

Mgeni Rasmi Mhandisi Pascal Muragili kabla ya ziara ya wilayani Manyoni katika Halmashauri ya wilaya ya Itigi kutundika mizinga ya kisasa, alianza na kutembelea mabanda ya maonesho katika viwanja vya Bombadia mjini Singida leo asubuhi Mei 19, 2023. Katika picha yupo katika banda la Mfuko wa Uhifadhi wa milima ya Tao la mashariki akipatiwa maelezo na Afisa Mradi wa kanda ya kusini Bi Rosemary Boniphace, jinsi utunzaji na uzalishaji wa Asali kisasa unavyo fanyika. Kulia kwa Mgeni Rasmi ni Mkurugenzi wa Misitu na Nyuki nchini Bw Bivoyo Deusdedit.

Wameiomba serikali kuongeza kina cha bonde lililopo ili kutunza zaidi maji wakati wa kiangazi  na kuongezewa mizinga 300 katika mradi wao.

Mgeni Rasmi Mkuu wa wilaya Mhandisi Pascal Muragili alipokea maombi hayo na kuahidi atayafikisha serikalini ili yafanyiwe kazi.

Katika maonesho hayo ya maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani, yanayo fanyika kila Mei 20, wizara ya Maliasili na Utalii nchini ambayo imeandaa maonesho hayo mjini Singida katika viwanja vya Bombadia, imezialika baadhi ya taasisi za uwezeshaji wananchi kiuchumi ili kutoa elimu ya jinsi ya kutunza nyuki kisasa na kuzalisha Asali na mazao yake kibiashara. Katika picha ni banda la SIDO mkoani Singida wakishirikiana na GS1-Tanzania katika kutoa elimu kwa washiriki wa maonesho hayo.


Mwisho.

Post a Comment

0 Comments