TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

TABEDO INAVYO TEKELEZA AGIZO LA WAZIRI MCHENGELWA KUHUSU WAHITIMU VYUO VIKUU KUJIAJIRI SEKTA YA NYUKI.

Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe Mohamed Mchengelwa (kulia mwenye skafu) akiwa kwenye banda la maonesho la Jukwaa la Ufugaji Nyuki (TABEDO) kwenye maonesho ya maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani yaliyomalizika hivi karibuni mkoani Singida. Waziri alimwagiza Mwenyekiti wa TABEDO Bi Rudia Hamudu (kushoto mwenye T-shirt ya njano) kuendeleza jitihada za kuwakusanya vijana wahitimu wa vyuo vikuu ili serikali kwa kusaidiana na TABEDO iweze kuwapatia mafunzo ya kuwajengea uwezo zaidi ili waweze kujiajiri katika sekta ya nyuki.

Na Urban Epimark, SINGIDA

Maonesho ya maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani yaliyo fanyika mwaka huu  kitaifa mkoani Singida kuanzia Mei 18 hadi 21, 2023 yamekuwa ya mafanikio makubwa kwa jamii na sekta nzima ya misitu na nyuki kwa kutoa Elimu kwa njia ya makongamano na uoneshaji bidhaa kwenye maonesho.

Maadhimisho hayo yaliyoratibiwa vizuri na Wizara ya Maliasili na Utalii ikishirikiana vyema na wadau mbalimbali wakiwemo Mradi wa kuendeleza ufugaji nyuki nchini yaani BEVAC, Wakala wa kuendeleza misitu yaani TFS lakini pia Jukwaa la Ufugaji nyuki yaani TABEDO na zingine nyingi.

Katika makala hii fupi tutaangazia jinsi Jukwaa la Ufugaji Nyuki yaani TABEDO linavyo tekeleza kwa vitendo dhima ya kushirikishana kwa wahitimu wa vyuo vikuu nchini katika kujiajiri hususani kupitia tafiti zao wanazo fanya wakiwa vyuoni lakini pia kwa kuzingatia agizo la Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe Mohamed Mchengelwa kuwezesha vijana kujiajiri.

Hotuba ya Mgeni Rasmi siku ya kufunga maonesho hayo ya maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani ambae alikuwa ni Waziri mwenye dhamana na Maliasili na Utalii nchini Mhe Mohamed Mchengelwa katika maagizo yake kwa watendaji wa wizara, alisisitiza kwamba 

"Ipo fursa kubwa ya vijana wanao hitimu vyuo vikuu kuweza kujiajiri katika sekta ya misitu na nyuki kwani bidhaa zitokanzo na mdudu nyuki ikiwemo Asali zinahitajika kwa kiwango kikubwa duniani na kutoa rai kwamba vijana wasaidiwe wajikusanye, watengeneze vikundi na serikali kupitia Wizara ikisaidiana na Jukwaa la Ufugaji Nyuki (TABEDO) iweze kuwajengea uwezo ili wajiajiri katika sekta ya Nyuki"


Mwenyekiti wa TABEDO Bi Rudia Hamudu (mwenye T-shirt ya njano) akiwa na baadhi ya wageni alio andamana nao kutembelea banda la kikundi cha Singida Beekeepers kwenye maonesho ya Siku ya Nyuki Duniani yaliyo malizika mkoani Singida. Mkurugenzi Mtendaji wa kikundi hicho Bw Yasini Masenga (kulia aliyevaa karabashia) ni mhitimu wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) mwenye Shahada ya Ecologia aliye hitimu mwaka 2020 na kujiajiri kupitia utafiti alio ufanya kwenye sekta ya Nyuki mkoani Singida na sasa anazalisha bidhaa za tiba mbadala kupitia masalia ya nyuki walio kufa.

Maagizo haya Waziri Mchengelwa aliyatoa mapema kwa Mwenyekiti wa TABEDO wakati alipotembelea banda la TABEDO na kumtaka Mwenyekiti wake Bi Rudia Hamudu kuhakikisha anaongeza idadi ya vijana walio jiajiri katikavsekta ya nyuki hadi sasa ambao ni takribani elfu 50 ambao Waziri alisema, hawatoshi.

"Serikali itaisadia TABEDO kuwajengea uwezo vijana ambao katika sensa ya watu ya mwaka 2022, imegundulika ni zaidi ya nusu ya watanzania wote hivyo, suluhisho kwa wao kupata mahitaji yao ni kujiajiri katika sekta ya nyuki" alisema Mhe Waziri Mchengelwa. 

Nae Mwenyekiti wa Jukwaa la Nyuki nchini (TABEDO) Bi Rudia Hamudu anasema, tayari Jukwaa hilo limeshaanza kutekeleza maagizo hayo ya serikali kwa kusaidiana na wadau mbalimbali kuhakikisha vijana kutoka vyuo vikuu wanajiahiri kupitia sekta ya nyuki.

Bi Rudia anasema, katika dhima nzima ya kushirikishana, TABEDO inashirikiana vyama, taasisi  na wadau wengine kuwajengea uwezo wanachama wake wakiwemo vijana baada ya kujiunga TABEDO ili kujifunza jinsi ya kuandaa vifaa stahiki vya kufugia nyuki, jinsi ya kuvuna Asali na kuisindika na kisha kuiweka kwenye vifungashio sahihi na kuziwekea alama za ubora pamoja na Barcodes.


Mwenyekiti wa TABEDO Bi Rudia Hamudu akiwa amesimama na Mkurugenzi Mwendeshaji wa kikundi cha ufugaji nyuki cha Bee Place Bi Salama Jima (mwenye blaus nyeupe pembeni) ambae pia ni mhitimu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na kujiajiri, wakimsikiliza Afisa mapokezi na mauzo wa kikundi hicho cha Bee Place Bi Rukia Hamis (mwenye ushungi kushoto) jinsi anavyo waelezea waliofika bandani hapo kuhusu ubora wa bidhaa za nyuki kutoka kikundi cha Bee Place kwenye maonesho ya Siku ya Nyuki Duniani mjini Singida.

Amelitaja Shirika la  kuendeleza viwanda vidogo vidogo  nchini yaani SIDO, lenye jukumu la kuwapatia wazalishaji wadogo ujuzi na maarifa ya kuandaa vifaa/mizinga, kuwafundisha jinsi ya kuitundika na kuvuna mazao ya nyuki kwa kuwajengea uzoefu na kuwaelekeza kwenye matumizi ya  teknolojia sahihi na rahisi itakayo wapatia tija zaidi.

Ameitaja taasisi nyingine ya GS1-Tanzania ambayo umuhimu wake kwa Jukwaa  la Nyuki (TABEDO) ni kuzipatia ithibati ya Msimbomilia kwenye bidhaa yaani Barcodes baada ya kuzifungasha kitaalumu ili  kusaidia kuzitangaza kwenye masoko ndani na nje ya nchi kwa mifumo ya kidigitali.

TABEDO pia inahakikisha inawawezesha wanachama wake kushiriki katika maonesho mbalimbali na kwenye makongamano ambayo yanalenga kukuza zaidi ujuzi na utaalam wa kuzaliza bidhaa bora zenye ushindani sokoni na kuongeza pato la mtu mmoja mmoja na pia kwa Taifa.

Wakitoa ushuhuda wa jinsi TABEDO imekuwa ikisaidia vijana baada ya  kuhitimu mafunzo yao vyuo vikuu ili kujiajiri na haswa kutokana na tafiti wanazo fanya, Mkurugenzi mwendeshaji wa kikundi cha Singida Beekeepers Bw Yasini Masenga ambae ni mhitimu kutoka Chuo Kikuu cha Dodona (UDOM) na mwenye shahada ya Biology  anasema,


Menyekiti wa TABEDO Bi Rudia Hamudu (kulia) akionesha moja ya bidhaa za kampuni ya Justin Natural Honey ya kutoka mkoani Iringa inayo milikiwa na kijana wa kitanzania mhitimu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambae amevalia T-shirt ya bluu kushoto (jina halikupatikana mara moja) kwenye maonesho ya Siku ya Nyuki Duniani yaliyo malizika hivi karibuni mjini Singida.

"Mimi ni mhitimu wa UDOM mwaka 2020 katika kitivo cha Biology. Nilipo kuwa chuoni nilifanya utafiti wa kuhusu nini faida za mdudu nyuki katika mkoa wetu wa Singida na hivyo kuvutiwa sana na sekta hii na hivyo kutaka kuendelea zaidi kujikita katika sekta hii ili kujiajiri" anaeleza Bw Yasini.

Yeye anaishukuru TABEDO kwa kumwonesha njia ya jinsi ya kujiajiri lakini pia anaushukuru mradi wa kuendekeza ufugaji nyuki kwa njia ya kisasa na kuzalisha Asali kibiashara wa BEVAC ambao wao kwa pamoja ndio wamemfikisha alipo sasa na kuweza kujiajiri.

Singida Beekeepers inatengeneza bidhaa za dawa za tiba mbadala kwa kutumia Masalia ya nyuki walio kufa, na pia kujishughulisha na ufugaji nyuki, uchakataji wa Asali na ufungashaji wake, ujuzi ambao ameupata kutoka SIDO. 

Mwingine mwenye ushuhuda kama huo ni Bi Salama Jima ambae pia ni mhitimu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambae ni Mkurugenzi Mwendeshaji wa kampuni yake ya  Bee Place inayo jishughulisha na uuzaji wa bidhaa za nyuki,  vifaa vya uvunaji asali na mengine mengi.


Mwenyekiti wa TABEDO Bi Rudia Hamudu kwenye maonesho ya Siku ya Nyuki Duniani yaliyo malizika mkoani Singida, alitumia muda mwingi kuwaelezea watu mbalimbali walio fika kwenye maonesho hayo jinsi vijana wa kitanzania wahitimu vyuo vikuu jinsi wameweza kuwa na uthubuti wa kujiajiri katika sekta ya nyuki badala ya kungojea ajira kutoka serikalini ambazo ni chache. Katika picha Bi Rudia anamwelezea mmoja wa walio fika kwenye banda la Bee Place na kujionea aina za vifaa za urinaji asili kwa njia ya kisasa.

Bi Salama anaishukuru TABEDO kwa kumlea na kumtafutia fursa za kujijengea uwenzo hadi kujiajiri mfano SIDO na taasisi zingine na pia kwenye makongamano mbalimbali na maonesho ya biashara, ameeleza Bi Salama.

Katika kuhitimisha makala hii, Mwenyekiti wa TABEDO Bi Rudia Hamudu anatoa wito kwa vijana wote nchini, kuitumia vyema fursa ya kujiajiri kupitia sekta ya nyuki. 

Lakini pia amesema, agizo la Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe Mohamed Mchengelwa la kuitaka TABEDO kukusanya vijana wengi zaidi ili wizara iweze kuwajengea uwezo, kwamba TABEDO itajipanga vyema zaidi kulitekeleza na pindi maadhimisho ya Siku ya Nyuki Duniani mwakani 2024,  yatakayo fanyika mkoani Dodoma pawepo na hatua kubwa ya mafanikio zaidi kwa vijana kujiajiri kuptia sekta ya nyuki baada ya kuhitimu vyuo vikuu.


Jukwaa la Ufugaji Nyuki (TABEDO) lina shirikiana kwa karibu na taasisi zingine katika kuwajengea uwezo vijana wahitimu vyuo vikuu ili kupata uelewa zaidi katika masuala ya usindikaji bora wa bidhaa ikiwemo mazao ya nyuki na pia jinsi ya kuzifungasha ili zipate wateja wengi sokoni. Katika picha, Afisa maendeleo ya Biashara wa SIDO mkoa wa Singida Bw Joel Tangai (kulia) akimwelezea mmoja ya walio fika katika banda la SIDO kwenye maonesho ya Siku ya Nyuki Duniani yaliyo malizika hivi karibuni mkoani Singida. Mbali na SIDO kuwasaidia vijana kujenga uwezo, ipo pia taasisi ya GS1-Tanzania inayo husika na utoaji wa Barcodes (Msimbomilia) kwa bidhaa zote zinazo zalishwa nchini yakiwemo mazao ya nyuki mfano Asali, Nta, Chavua ili ziweze kujitangaza zaidi na kupata masoko ndani na nje ya Tanzania.


Mwisho.

Post a Comment

0 Comments