TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

GEITA WAANZA KUTEKELEZA MAELEKEZO YA WARAKA WA ELIMU KUMLINDA MTOTO NA UKATILI

Mkuu wa dawati la Jinsia wanawake na watoto wilaya ya Geita Christina Katana akizungumza na wanafunzi wa shule ya msingi Mwangimagi mjini Geita. 

Salum Maige,Geita.

Februari 28,mwaka huu serikali kupitia wizara ya elimu sayansi na teknolojia ilitoa waraka wa elimu Na.01 wa mwaka 2023 kuhusu uboreshaji wa huduma ya mabasi yanayotumika kusafirisha wanafunzi kuwa na watoa huduma wawili wa kike na wakiume ikiwa ni mkakati wa kudhibiti unyanyasaji na ukatili kwa watoto.

Hatua hiyo ya serikali ni baada ya kutokea kwa matukio ya unyanyasaji yanayodaiwa kufanywa na makonda na madereva kwa wanafunzi wanaosoma shule zinazotoa huduma ya usafiri wa mabasi hivyo wizara hiyo ikatoa maelekezo kwa wamiliki wa shule kuhakikisha mabasi yanakuwa na wahudumu hao.

Matukio yaliyoripotiwa ni madai ya baadhi ya makonda,madereva na watoa huduma wa mabasi hayo kuwafanyia ukatili wa kingono baadhi ya wanafunzi wanapowarudisha nyumbani hasa nyakati za jioni.

Katika mkoa wa Geita tayari kuna hatua mbalimbali zimeanza kuchukuliwa za kuhakikisha maelekezo yaliyotolewa kupitia waraka huo yanazingatiwa ikiwa ni pamoja na kuanza kutoa elimu kwa wamiliki wa shule wanaotoa huduma ya usafiri kwa wanafunzi pamoja na waratibu elimu kata.

Akizungumzia hatua hizo Mkuu wa kikosi cha usalama barabarani mkoa wa Geita Nelson Ndifwa amesema, amezunguka wilaya zote tano za mkoa wa Geita na kufanya vikao vya kutoa elimu kuhusu utekelezaji wa agizo la serikali la kuhakikisha mabasi yanakuwa na watoa wawili wa kike na kiume.

Amesema ,kabla ya kufunguliwa shule julai 3,mwaka huu kutafanyika ukaguzi wa magari yote yanayotoa huduma hizo yanakuwa na rangi za njano,watoa huduma wawili,viti kuwa na mikanda kwa ajili ya usalama wa watoto.

Kadhalika,ameongeza kuwa jeshi la polisi kitengo cha usalama barabarani litahakikisha mtoto anatoka na kurudi nyumbani akiwa salama bila kunyanyaswa au kufanyiwa ukatili wa namna yoyote.

Na niwaonye tu wamiliki wa shule ,mtoto kusimama ndani ya gari sio kitendo kizuri,tumeshatoa maelekezo kwa wamiliki wa shule kuhakikisha magari yote yanakuwa na mikanda na watoto wakae kulingana na viti vilivyomo sio kubeba zaidi ya uwezo wa gari”,anasema Ndifwa.

Katika kuhakikisha usalama wa mtoto unafuatwa ,ameshauri kuwa,kila shule kuwa na afisa usafirishaji atakayekuwa anaratibu masuala ya usafiri kila siku kwa kuzingatia ratiba ya safari za watoto na kwamba mtu huyo atahakikisha magari hayo yanafanyiwa ukaguzi kila wakati.

Afisa huyo pia atakuwa na kazi ya kuhakikisha gari linaloondoka kwenda kuchukua watoto na kupeleka watoto nyumbani linakuwa na watoa huduma wawili,huwezi kusajili wanafunzi wengi halafu ukawa na magari machache,tutafuatilia kila hatua ,jambo la kuwalundika watoto kwenye gari ni ukatili ambao haukubaliki pia”anasema Ndifwa.

Mkuu wa dawati la jinsia,wanawake na watoto wilaya ya Geita mkaguzi msaidizi wa Polisi Christina Katana amevitaja viashiria vilivyoonekana na kusababisha serikali kutoa waraka huo ni kunyanyasika kwa watoto hasa mtoto kwanza kuingia kwenye gari na wa mwisho kushuka.

Mtoto wa kwanza kuingia kwenye gari ndiye anakuwa hatarini zaidi kufanyiwa unyanyasaji na ukatili kwani anachukuliwa nyumbani mapema,na mtoto wa mwisho anazungushwa kwenye gari zaidi ya masaa mawili hadi jioni naye yupo kwenye wakati mbaya wa kufanyiwa vitendo hivyo”anasema Katana.

Ameongeza kuwa, kitu kinachokwaza wapinga ukatili na unyanyasaji dhidi ya watoto ni idadi kubwa ya watoto wanaobebwa kwenye gari na kusababisha watoto wakati mwingine kubebana na kusimama ndani ya gari kitendo ambacho ni kumnyanyasa na kumkatili mtoto.

Kamishna wa Elimu Tanzania Dk.Lyabwene Mtahabwa

Sisi wapinga ukatili ,tunaipongeza sana serikali kuja na waraka huu wa kuhakikisha mabasi ya wanafunzi yanakuwa na watoa huduma wawili kwani kabla kulikuwa na matukio hayo ya unyanyasaji na ukatili,na kwamba sisi tupo pamoja kuhakikisha maelekezo yaliyomo kwenye waraka huo yanazingatiwa. 

Mwalimu mkuu wa shule binafisi ya msingi ya True Vision,Octavian Mutta amethibitisha kupokea waraka wa elimu uliotolewa kwa lengo la kudhibiti unyanyasaji kwa wanafunzi.
Anasema ,wao kama walengwa wakuu wa utekelezaji wa agizo hilo tayari wameanza kutekeleza wiki mbili kabla ya likizo ya mwezi wa sita kuanza.
Tunashukuru serikali kutoa elimu kwa wamiliki wa shule kuhakikisha maelekezo yaliyotolewa na wizara yanafuatwa ili kupunguza vitendo viovu vya unyanyasaji na ukatili,elimu iliyotolewa na maofisa ustawi wa jamii,maofisa meaendeleo ya jamii pamoja na jeshi la polisi sisi kama wamiliki wa shule tutazingatia” anasema Mutta.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Shirika lisilokuwa la kiserikali la kupinga ukatili dhidi ya watoto na wanawake(NELICO) Paulina Alex ametaja ukatili wanaofanyiwa watoto kuwa, ni pamoja na kulundikwa kwenye magari na kulazimishwa kusukumaa magari ya shule pindi yanapoharibika njiani.

Akizungumzia waraka huo anasema,moja ya haki ya mtoto ni kupata elimu bora kwa mazingira bora likiwemo suala usafiri na kwamba kila mtu kwa nafasi yake ahakikishe mtoto hakumbani na ukatili au unyanyasaji wowote akiwa ndani ya gari au nje ya gari.

Sisi kama NELICO hatukubali kuona haki za mtoto zikikanyagwa hata kidogo,tutafuatilia kwa sababu ni sehemu ya majuku yetu ya kumlinda mtoto.Nipongeze tu jeshi la polisi kwa hatua zinazochukuliwa na kusimamia watoto kuvuka barabara,lakini nilipongeze juhudi zake za kudhibiti wimbi la ubebaji watoto kupita kiasi”anasema Alex.

Mmoja wa wanafunzi wanaotumia usafiri wa gari kwenda shule,ambaye jina lake linahifadhiwa amesema ,kuna wakati gari analopanda hubeba wanafunzi wengi hali inayosababisha baadhi ya watoto kuchoka na kuanza kusinzia ndani ya gari.

Tunabebwa wengi sana kwenye gari,tunachoka kwa kusimama,kubebena”anasema mwanafunzi huyo mwenye umri wa miaka nane anayesoma darasa la tatu jina la shule linahifadhiwa.

Kwa mujibu wa waraka huo uliosainiwa na kamishna wa elimu Tanzania Dk.Lyabwene Mtahabwa ,unaeleza kwamba thamani ya rasilimali watoto ni kubwa kuliko thamani ya rasilimali yoyote ambayo tumejaliwa kuwa nayo katika nchi.

Pamoja na ukweli huo,imebainika kuwa baadhi ya watoa huduma kwa watoto wamekuwa na tabia zenye mwelekeo wa kuleta mmomonyoko wa maadili,kuathiri ukuaji,ujifunzaji na kuhatarisha ustawi wa watoto kwa ujumla.

Waraka huo ulioanza kutumika machi 1,mwaka huu unawataka wamiliki wa shule wahakikishe wanakomesha vitendo vya ukatili kwa wanafunzi wakiwa kwenye magari au mabasi,kuwa na ratiba rafiki za safari ili wanafunzi,hususani watoto wadogo wapate muda wa kutosha kupumzika kwa ajili ya ukuaji wao.

Wanafunzi wakisongamana kuingia kwenye basi la shule

Pia,waraka huo huo umepiga marufuku kuweka miziki au nyimbo na picha za video zinazokwenda kinyume na maadili,mila,desturi na tamaduni zetu na badala yake kuweka miziki au nyimbo na picha za video zinazojenga maadili na uzalendo wa wanafunzi. 

Kwa mujibu wa takwimu zinazotokana sense ya watu na makazi ya mwaka 2022 watoto wenye umri wa kuanzia mwaka 0-4 ni watoto 9,484,170,watoto wenye umri wa kuanzia miaka 5-9 ni watoto 8,918,580 huku watoto wa mwaka 0-14 wakiwa ni asilimia 42.76.
Mwisho

Post a Comment

0 Comments