TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

IRDP NA MBOGWE DC WAFANYA BONANZA LA MICHEZO KUKUZA USHIRIKIANO.

Mgeni Rasmi Mkuu wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) Prof Hozen Mayaya (pichani) akiongea wakati wa ufunguzi wa Bonanza hilo jijini Dodoma Juni 06, 2023

Na Urban Epimark, DODOMA.

Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) pamoja na Halmashauri ya wilaya ya Mbogwe (Mbogwe DC) kutoka mkoani Geita wamefanya bonanza la michezo kuimarisha afya ya mwili na kukuza zaidi ushirikiano baina yao.

Bonanza hilo lililo fanyika jijini Dodoma Juni 06, 2023 katika viwanja vya Shule ya Sekondari ya John Merlin lilishirikisha michezo mbalimbali kwa wanawake na wanaume ikiwemo riadha, kuvuta kamba, mpira wa Pete, mpira wa miguu, kukimbiza kuku na mingine mingi.

Akizungumza wakati wa ufungunzi wa Bonanza hilo Mgeni Rasmi  Mkuu wa Chuo cha Mipango na Maendeleo Vijijini (IRDP) Prof Hozen Mayaya alizipongeza taasisi zote mbili pamoja na watumishi wote kwa kutambua faida za kufanya mazoezi ya kujenga afya ya mwili lakini pia kukuza mhusiano baina ya taasisi hizo.

Mgeni Rasmi katika Bonanza hilo Mkuu wa Chuo cha Mipango Prof Hozen Mayaya (katikati) akiwa na wageni wengine pamoja na wachezaji wa timu ya mpira wa Pete (wanawake) kutoka wilayani Mbogwe mkoani Geita wakati wa Bonanza hilo jijini Dodoma Juni 06, 2023. Mwanzo kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko wa IRDP Bw Godrick Ngolly.

"Kwetu sisi kutembelewa na wenzetu wa Halmashauri ya wilaya ya Mbogwe (Mbogwe DC) na kufanya Bonanza hili, ni jambo kubwa na jema kwani tutaweza kuboresha zaidi afya zetu na pia kufahamiana na kujenga mahusiano mazuri katika majukumu yetu" alisema Prof Mayaya

Pia Prof Mayaya aliendelea  kufafanua kwamba IRDP itaenda pia wilayani Mbogwe kuendesha mafunzo kwa Watendaji wa Vijiji na Kata na kusaidia kuitengenezea Halmashauri hiyo "Social Economic Profile" pamoja na kufanya michezo mbalimbali, aliongeza kwa kusema hivyo.

Mgeni Rasmi katika Bonanza hilo Mkuu wa Chuo cha Mipango Prof Hozen Mayaya akifurahia jambo wakati alipokuwa akiongea na washiriki wa Bonanza la IRDP na Mbogwe DC lililo fanyika jijini Dodoma Juni 06, 2023. Aliye shikilia kipaza sauti kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko wa Chuo cha Mipango (IRDP) Bw Godrick Ngollly.

Kwa upande wa Halmashauri ya wilaya ya Mbogwe, Kaimu Mkurugenzi ambae pia ni Afisa Utumishi wa Wilaya ya Mbogwe Bw Sospeter Mshamba alisema kuwa Chuo cha Mipango kimekuwa kikitoa wataalamu katika fani mbalimbali za mipango ambazo husaidia sana katika kuleta maendeleo katika maeneo ya kazi.

"Tuna ushukuru uongozi wa Chuo cha Mipango kwa kukubali ombi letu la kusaidiwa kuandaa "Social Economic Profile" kwa ajili ya wilaya yetu ya Mbogwe ambayo kwa sasa hatuna" alieleza Afisa Utumishi Bw Sospeter Mshamba.

Mbunge wa Jimbo la Mbogwe Mhe Nicodemus Maganga akiongea wakati wa Bonanza hilo jijini Dodoma Juni 06, 2023. Anae shuhudia mazungumzo hayo ni Mgeni Rasmi katika Bonanza hilo Prof Hozen Mayaya, mwanzo kabisa kushoto. Aliye shikilia kipaza sauti kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko wa Chuo cha Mipango (IRDP) Bw Godrick Ngolly.

Nae Mbunge wa Jimbo la Uchaguzi la Mbogwe mkoani Geita Mhe Nicodemus Maganga (CCM) ambae alihudhuria pia Bonanza hilo alilisisitiza wafanyakazi wote nchini kuzingatia utaratibu wa kupenda  michezo ili kuepukana na magonjwa yasiyo ambukiza.

Alitaja magonjwa hayo  kama vile magonjwa ya moyo, mkandamizo wa damu ya presha, kisukari na mengineyo na kusisitiza waige mfano wa Chuo cha Mipango na wenzao kutoka Halmashauri ya wilaya ya Mbogwe.

Timu za mpira wa miguu zilizo chuwana baina ya Chuo cha Mipango (IRDP) na Mbogwe DC wakiwa kwenye mpambano uwanjani katika Shule ya Sekondari ya John Merlin ya jijini Dodoma Juni 06, 2023.

Katika michezo iliyo fanyika, matokeo ya kuvuta kamba wanaume, ushindi ulienda kwa Chuo cha Mipango kwa kupata mivuto miwili kwa bila dhidi ya wanaume wa Mbogwe DC.

Riadha mita 100  kwa wanaume mshindi wa kwanza hadi wa tatu  walitoka Mbogwe DC na kwa upande wa mchezo wa mpira wa Pete, Chuo cha Mipango walipata vikapu18 dhidi ya wanafunzi walio pata 13, mpira wa miguu baina na wenyeji Chuo cha Mipango na wageni Mbogwe DC wali toshana nguvu.

Timu za mpira wa Pete baina na Chuo cha Mipango (IRDP) na Mbogwe DC wakiwa uwanjani wakioneshana uwezo kwenye viwanja vya shule ya sekondari ya John Merlin ya jijini Dodoma Juni 06, 2023.


Mwisho.

Post a Comment

0 Comments