TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

ICAP YAKABIDHI PIKIPIKI NA VIFAA TIBA VYENYE THAMANI YA ZAIDI YA TSH. MILIONI 186,900,000 MKOANI GEITA ILI KUIMARISHA HUDUMA ZA AFYA

 

Na Theresia Method;

Taasisi ya ICAP, kwa ufadhili wa serikali ya Marekani kupitia mradi wa CDC na PEPFAR, imekabidhi pikipiki 50 na vifaa tiba joto sita (thermocoagulators) vya kupima saratani ya mlango wa kizazi kwa wanawake kwa serikali ya mkoa wa Geita ili kuboresha huduma za afya.

Hafla  ya makabidhiano ya vifaa hivyo  imefanyika leo 14 Januari 2025 katika ofisi za ICAP mjini Geita.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mheshimiwa Martine Shigela ambaye ni mkuu wa mkoa wa Geita ameishukuru taasisi ya ICAP na serikali ya Marekani  kwa msaada wao endelevu katika mapambano dhidi ya saratani ya shingo ya kizazi na UKIMWI.

"Msaada huu ni muhimu sana katika kuboresha huduma za afya vijijini, na tuna imani kwamba utaongeza kasi ya upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wanawake," alisema Shigela.


Shigela alisema, hatua hii nimatokeo ya ushirikiano ambao unafanywa na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na serikali ya Marekani hasa katika kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Naibu Mkurugenzi Mkazi ICAP Tanzania Dr John Kahemele (wa kwanza kutoka kulia) akikabidhi pikipiki kwa Mkuu wa Mkoa wa Geita.

Mkuu wa mkoa wa Geita wa tatu kutoka kushoto akipokea box la vifaa tiba joto kutoka kwa Naibu mkurugenzi Mkazi ICAP Tanzania.

Naibu Mkurugenzi Mkazi wa ICAP Tanzania Dk. John Kahemele, alieleza kuwa vifaa hivi ni vya kisasa na vina uwezo wa kutoa matibabu kwa usahihi zaidi bila kuwa na changamoto yoyote

Alisema katika kipindi cha mwaka jana 2024, jumla ya wanawake elfu 27 walifikiwa na kwa mwaka huu 2025 malengo ni kuwafikia wanawake elfu 35 huku wanawake 515 wakipatiwa matibabu ya saratani ya awali ya mlango wa kizazi kwa mwaka huo wa 2024.

"Teknolojia hii mpya itaongeza uwezo wetu wa kuwahudumia wanawake wengi zaidi hasa wale walioko maeneo ya vijijini ambako upatikanaji wa huduma za afya umekuwa changamoto," alisema Dk. Kahemele.


Naibu Mkurugenzi Mkazi ICAP Tanzania Dr John Kahemele (wa kwanza kutoka kulia)                                  akielezea faida zitakazotokana na msaada waliotoa.

Aidha shughuli hii imeonesha dhamira ya dhati ya ICAP katika kusaidia kupambana na UKIMWI na saratani ya shingo ya kizazi, ikiimarisha huduma za kinga na tiba kwa wanawake. Hii ni hatua muhimu katika kuhakikisha wanawake wanapata huduma bora za afya na kuzuia vifo vinavyoweza kuzuilika.

Kupitia hafla hiyo kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Geita kamishina msaidizi mwandamizi wa polisi Safia Jongo aliiomba taasisi ya ICAP kuongeza nguvu katika upatikanaji wa usafiri ili kuwawezesha askari wa jeshi la polisi hasa kitengo cha dawati la jinsia na watoto kuwafikia kwa wakati wahanga wa matukio ya ukatili

Kamanda Jongo alisema maeneo mengi ya vijijini ufikikaji umekuwa mgumu,hivyo ICAP walichukue suala hilo kama changamoto inayohitaji ufumbuzi

“Tunawashukuru ICAP kwa kutoa usafiri huu na vifaa tiba, lakini na mimi pia nitumie nafasi hii kuwaomba mtuunge mkono katika kupata usafiri wa uhakika kwaajili ya kuwafikia wahanga wa matukio ya ukatili hususani wale waliopo maneo ya vijijini”. Alisema Kamanda Jongo

 

 

kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Geita kamishina msaidizi mwandamizi wa polisi Safia Jongo pamoja na katibu tawala mkoa wa Geita  Mohamed Gombati wakiwa katika hafla ya makabidhiano ya pikipiki na vifaa tiba.

Post a Comment

0 Comments