TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

BODI YA BIMA YA AMANA YANG’ARA MAONESHO YA NANE YA TEKNOLOJIA YA MADINI GEITA 2025.

Na Theresia Method-Geita;



Wawakilishi wa Bodi ya Bima ya Amana katika maonyesho ya nane  ya Teknolojia ya Madini kwa mwaka 2025 yaliyofanyika katika viwanja vya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Bombambili, mkoani Geita kwenye picha ya pamoja.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa, aliongoza uzinduzi wa Maonesho ya Nane ya Teknolojia ya Madini kwa mwaka 2025 yaliyofanyika katika viwanja vya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Bombambili, mkoani Geita, Septemba 22, 2025.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa, akihutubia umma katika uzinduzi wa Maonesho ya Nane ya Teknolojia ya Madini kwa mwaka 2025 yaliyofanyika katika viwanja vya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Bombambili, mkoani Geita.

Maonesho haya, yaliyoanzishwa mwaka 2018, yamejikita katika kuimarisha sekta ya madini nchini kwa kuhakikisha kuwa rasilimali za madini zinawanufaisha watanzania wote. Katika uzinduzi huo, Waziri Mkuu alisisitiza umuhimu wa kutumia teknolojia sahihi na kuwa na uongozi bora ili kufanikisha maendeleo endelevu katika sekta ya madini, sambamba na kuhamasisha ushiriki wa wananchi katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.


Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa akitembelea mabanda mbalimbali.

Maonesho hayo yamekuwa jukwaa muhimu la kukutanisha wadau mbalimbali wa sekta ya madini kutoka serikalini, sekta binafsi, wachimbaji wakubwa na wadogo, taasisi za fedha, wajasiriamali hadi wafanyabiashara. Kaulimbiu ya mwaka huu ilikuwa; “Ukuaji wa Sekta ya Madini ni Matokeo ya Matumizi ya Teknolojia Sahihi na Uongozi Bora, Shiriki Uchaguzi Mkuu  2025.”

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa akitembelea mabanda mbalimbali.

Siku moja kabla ya uzinduzi wa maonyesho hayo, Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Geita (Samwel Shoo),alieleza kuwa Tume ya Madini imeshiriki kwa mara ya nane mfululizo katika maonyesho hayo, ambapo mwaka huu iliandaa huduma za elimu kwa wadau wote kuhusu teknolojia za kisasa katika utafiti, uchimbaji na uchenjuaji wa madini.


Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Martine Shigela akiwa na Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Geita, Bw. Samwel Shoo siku moja kabla ya ufunguzi wa maonyesho hayo.

Katika maonesho hayo, Bodi ya Bima ya Amana (DIB) iliibuka kuwa miongoni mwa taasisi zilizovutia watu wengi kwa utoaji wa elimu muhimu kuhusu kinga ya amana kwa wateja wa benki na taasisi za kifedha. Bw. Nkanwa Magina, Mkurugenzi wa Kinga ya Amana na Uwekezaji wa DIB, alieleza kuwa bodi hiyo ilianzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Benki na Taasisi za Fedha ya mwaka 1991, na kuendelea kufanya kazi chini ya vifungu vya 36 hadi 42 vya Sheria ya Mwaka 2006, ikiwa na lengo la kuwalinda wateja wadogo dhidi ya kupoteza amana zao iwapo taasisi za fedha zitakumbwa na changamoto.

“Bodi hii ilianza rasmi mwaka 1994 kwa kazi kuu maalumu, moja ni kulipa fidia ya bima ya amana kwa kiwango cha shilingi milioni  saba na laki tano kwa kila mwenye amana katika kila benki au taasisi ya kifedha, na pili ni kujenga imani ya wateja katika mfumo rasmi wa kifedha nchini” alisema Bw. Magina .

Mapokezi kwa DIB katika maonesho hayo yalikuwa chanya sana. Wananchi wengi walitembelea banda hilo na kueleza kuridhishwa kwao na elimu waliyopewa. Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano wa Umma na Mawasiliano wa DIB, Bw. Lwaga Mwambande, alisisitiza kuwa taasisi hiyo itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa sekta ya fedha ili kuhakikisha huduma zake zinafika kwa Watanzania wengi zaidi, wakiwemo wale wanaotumia mifumo ya kifedha isiyo rasmi kama VICOBA na SACCOS.


Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano wa Umma na Mawasiliano wa DIB, Bw. Lwaga Mwambande akitoa elimu katika maonyesho hayo.

Mkuu wa Wilaya ya Geita, Hashim Komba, alitumia jukwaa hilo kutoa rai kwa DIB kuongeza juhudi za kupanua huduma zake hadi kwenye vikundi vidogo vya kifedha visivyo rasmi. 

“Watanzania wengi bado wanaweka fedha kwenye maeneo ambayo hayajasajiliwa rasmi, na hivyo kupoteza mamilioni ya shilingi wanapokumbwa na changamoto. Ni wakati sasa wa kuongeza kasi ya kulinda mitaji ya wananchi wetu,” alieleza DC Komba.

Kwenye majibu yake, Bw. Mwambande alisema DIB imeshapokea ushauri huo na itaendelea kuimarisha ushirikiano na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na taasisi nyingine ili kufikia kundi hilo kubwa la wananchi wanaotumia mifumo isiyo rasmi.

“Kinga ya Shilingi milioni 7.5 kwa kila mteja inatosheleza asilimia 99 ya wamiliki wa amana nchini. Lengo letu si tu kulipa fidia endapo benki itafungwa, bali kuhakikisha wananchi wana imani ya kudumu na mfumo rasmi wa kifedha,” alisema Bw. Mwambande.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Geita (RMO), Dkt. Omari Sukari, naye hakuachwa nyuma katika kutoa pongezi kwa Bodi ya Bima ya Amana kwa kushiriki maonesho hayo na kutoa elimu kwa jamii kuhusu usalama wa fedha zao. 

“Nimejifunza kwamba hata kama benki ikifilisika, fedha zangu ziko salama kwa sababu kuna bodi inayozilinda. Hii ni habari njema kwa Watanzania wote,” alisema Dkt. Sukari. mwenye shati la kitenge.

Aliipongeza DIB pia kwa kuanza kuchukua hatua za mapema kuokoa benki zinazopitia changamoto kabla hazijafungwa, jambo alilolielezea kuwa ni mwelekeo sahihi wa kujenga uthabiti wa sekta ya fedha nchini.


Mganga Mkuu wa Mkoa wa Geita (RMO), Dkt. Omari Sukari akisikiliza kwa makini elimu inayotolewa na timu ya wafanyakazi wa DIB

Wananchi wengi waliotembelea banda la DIB walieleza kufurahishwa na namna walivyopokelewa kwa ukarimu na kufundishwa kwa kina kuhusu namna fedha zao zinavyolindwa. Salama Aron, ni mmoja wa washiriki wa maonesho hayo, alisema “Nimejifunza kwamba fedha zetu benki zipo salama hata kama benki itafungwa. Tunalindwa na Bodi ya Bima ya Amana.”

Salama Aron mmoja wa washiriki aliyetembelea banda la DIB
Wanafunzi walipotembelea banda la DIB

Maonesho ya mwaka huu yalihitimishwa rasmi Septemba 28, 2025 na Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko, aliyesema maendeleo ya sekta ya madini nchini yameongeza masoko ya madini hadi kufikia 43 na vituo vya ununuzi kufika 109.


Muonekano wa baadhi ya vibanda kwenye Maonesho ya Nane ya Teknolojia ya Madini kwa mwaka 2025 yaliyofanyika katika viwanja vya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Bombambili, mkoani Geita.

Dkt. Biteko alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kuongeza ushirikishwaji wa Watanzania katika mnyororo mzima wa thamani ya madini kutoka kwenye utafiti, uchimbaji, uchenjuaji hadi biashara ya madini ili kuhakikisha rasilimali za taifa zinawanufaisha wananchi moja kwa moja.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko akihutubia wananchi wakati wa kufunga Maonesho ya Nane ya Teknolojia ya Madini kwa mwaka 2025 yaliyofanyika katika viwanja vya Dkt. Samia Suluhu Hassan, Bombambili, mkoani Geita.


Zaidi ya washiriki 900kutoka ndani na nje ya Tanzania walishiriki katika maonesho haya ya kihistoria, ambayo si tu yalionesha teknolojia mbalimbali, bali pia yamefungua fursa ya elimu, ushirikiano na ujenzi wa uchumi imara kwa Watanzania kupitia sekta ya madini na kifedha.


Post a Comment

0 Comments