TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

KAZI NA MATOKEO: MWANGA MPYA WA GEITA MJINI

Na Victor Bariety;

 

Kwenye siasa za ushindani mara nyingi mgombea anapokuwa hana mpinzani huwa ana nafasi ya kutulia, akingoja tu siku ya uchaguzi. Lakini hali ni tofauti kwa Eng. Chacha Mwita Wambura, Mgombea Ubunge wa Jimbo la Geita Mjini kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM). Pamoja na ukweli kwamba hakuna chama cha upinzani kilichojitokeza kupambana naye kwenye uchaguzi wa mwaka huu, bado ameamua kutembea kila kona ya jimbo akisikiliza kero na changamoto za wananchi wake. Hii ndiyo taswira ya kiongozi anayeamini kwamba kazi na matokeo havianzi baada ya kuapishwa, bali kabla hata ya kupigiwa kura.

 

Leo, Septemba 26, Eng. Chacha alishusha hatua zake katika Soko la Nyankumbu, akiambatana na mgombea udiwani wa Kata hiyo, Paschal Kimisha Sukambi, na viongozi wengine wa CCM Wilaya ya Geita. Ziara hiyo imegeuka kuwa kioo cha dhati cha dhamira ya viongozi hawa kwa wananchi, kwa kuwa haikuishia kwenye mikutano ya kampeni pekee bali ilijikita kwenye kusikiliza na kuandika moja kwa moja kero zilizowakumba wafanyabiashara wa eneo hilo.

 


Miongoni mwa changamoto zilizotolewa na wafanyabiashara wa Nyankumbu ni pamoja na:

Ukosefu wa maji ya kutosha kwenye vyoo vya soko;

Kukosekana kwa eneo maalum la kushushia mizigo;

Matizo la mitaro ya maji machafu, yanayohatarisha afya na usalama;

 


Malalamiko juu ya tozo za vizimba ambazo zinadaiwa kuwa kikwazo kwa wajasiriamali wadogo.

Badala ya kutoa majibu mepesi, Eng. Chacha aliwaeleza wafanyabiashara hao kwamba serikali ya CCM tayari imeweka mikakati kabambe ya kuhakikisha masoko yanakuwa na mazingira bora, salama na yenye tija kwa wafanyabiashara. Aliahidi kuwa, akipewa ridhaa ya kuwatumikia kama Mbunge, atashirikiana kwa karibu na viongozi wa serikali na taasisi husika kuhakikisha changamoto hizo zinapata suluhisho la kudumu, huku akisisitiza kuwa Soko la Nyankumbu linastahili kuboreshwa kwa viwango bora kulingana na mpango wa kitaifa wa kuboresha masoko.

 

Lakini picha ya uongozi wa vitendo haikuishia kwa Eng. Chacha pekee. Paschal Kimisha Sukambi, mgombea udiwani wa Kata ya Nyankumbu, ameonyesha namna siasa za karibu na wananchi zinavyoweza kufanyika kwa unyenyekevu. Badala ya mikutano mikubwa pekee, Sukambi amekuwa akipita nyumba kwa nyumba, akisalimia wakazi wake na kuandika kwenye daftari maalum kero wanazomweleza. Kauli yake ni rahisi: “Nikitunukiwa udiwani, nataka nianze kazi nikijua pa kuanzia, kwa sababu changamoto zenu ndizo dira yangu.”

 


Kwa mtazamo wa wengi, mshindi wa kweli wa uchaguzi si jina litakalotangazwa na Tume ya Uchaguzi, bali ni yule ambaye wananchi wameshajionea kwa macho yao kwamba ana dhamira, uchapa kazi na msukumo wa kuleta matokeo. Na kwa dalili hizi, wakazi wa Geita wanashuhudia taswira hiyo mapema.


Kuna methali isemayo, dalili ya mvua ni mawingu. Hali ya sasa ya Eng. Chacha na Sukambi ni mawingu yenye mvua ya matumaini. Wanaonyesha kwamba siasa siyo ahadi za majukwaani pekee, bali ni kusikiliza, kuandika na kutenda. Wameweka mizizi ya uongozi wa karibu na wananchi kabla hata ya kupewa dhamana rasmi.

 


Wananchi wa Geita wanayo nafasi kubwa Oktoba hii ya kuamua mustakabali wa maendeleo yao. Na iwapo watachagua viongozi wanaosimama kwenye msingi wa kazi na matokeo, basi jimbo hili litakuwa darasa la mfano kwa nchi nzima.

 

Mwisho 

Imeandaliwa na Victor Bariety

0757-856284

 PICHA ZAIDI








Post a Comment

0 Comments