TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

MIRADI YA TARURA GEITA YACHONGEA WAPINZANI: MWENGE WA UHURU WAIPA HESHIMA BARABARA YA NYAKAFURU

Na Victor Bariety-Geita;


Mkoa wa Geita unaendelea kujipambanua katika ubora wa utekelezaji wa miradi ya miundombinu, baada ya barabara ya Nyakafuru, iliyojengwa kwa kiwango cha lami nyepesi, kutajwa kama mradi wa mfano kupitia mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025.

 

Barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 0.7, inayojengwa na mkandarasi Rumanyika Investment Co. Ltd wa Karagwe kwa gharama ya zaidi ya shilingi milioni 569, imekuwa tumaini jipya kwa wakazi wa Masumbwe na wachimbaji wadogo wa dhahabu waliokuwa wakikabiliwa na changamoto kubwa za usafiri. Mradi ulianza Agosti 2024 na unatarajiwa kukamilika Septemba 2025, chini ya usimamizi wa TARURA Wilaya ya Mbogwe.

 


Ukaguzi wa kifedha na kiufundi bila doa

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Ismail Ali Ussi, ameongoza ukaguzi wa kina kwa kutumia mitambo ya kisasa na kupitia nyaraka zote za utekelezaji. Baada ya ukaguzi huo, alisifu ubora wa kazi na kueleza wazi kuwa mradi huo hauna doa.


 “TARURA mmeweka alama nyingine kubwa. Huu ni uthibitisho kwamba fedha za umma zikitumika ipasavyo, wananchi wananufaika kwa vitendo,” amesema Ussi.

 


Wachimbaji wafunguka hisia zao

 

Wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi, wachimbaji wadogo wa Nyakafuru walifurika wakishangilia, wakisisitiza kuwa mradi huo umewafungulia ukurasa mpya wa maisha.


Masumbuko Ibazu, mchimbaji mdogo, amesema kwa msisitizo:

 “Barabara hii ilikuwa kero kwa miaka mingi. Tulipata mateso kusafirisha mawe na tulilipa gharama kubwa sana. Marais walipita wakiahidi, lakini hakuna aliyetekeleza. Leo mama Samia ametutengenezea barabara ya ndoto. Wachimbaji wa Nyakafuru tunasema wazi – wapinzani wasijaribu kusogelea huku. Hii ni barabara ya wananchi, ni barabara ya maendeleo. Hatutaki maneno ya upinzani, tunataka vitendo kama hivi.”

 


Naye Kahigi Jeremiah aliweka wazi hisia za wengi:

 “Mama ni mama tu, anajua uchungu wa watoto wake. Ametunyamazisha kwa vitendo, siyo maneno. TARURA wamefanya kazi kubwa na wamewachongea wapinzani kwa wachimbaji. Nyakafuru sasa ni ngome ya maendeleo – hakuna nafasi ya wapinzani.”

 

Fursa za kiuchumi na kijamii

Meneja wa TARURA Mbogwe, Mhandisi Patrick Chacha, alibainisha kuwa barabara ya Nyakafuru haitabaki kuwa alama ya usafiri pekee, bali ni kichocheo cha maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

 “Barabara hii inarahisisha usafirishaji wa watu na mazao, inafungua uwekezaji mpya na inachochea ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla,” amesema.

 


Taswira ya Geita yazidi kung’ara

Barabara ya Nyakafuru imekuwa mradi wa nne mfululizo kukaguliwa na Mwenge wa Uhuru ndani ya siku nne bila kubainika kasoro, baada ya barabara ya Nzera, barabara ya Kasco na daraja la Kharumwa–Nyijundu.




Mfululizo huu wa mafanikio umeimarisha taswira ya Geita kitaifa, tofauti na miaka iliyopita ambapo baadhi ya miradi ya Mwenge ilikataliwa kutokana na dosari. Safari hii, miradi ya TARURA Geita imekuwa kioo cha mfano, ikionesha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan.

 


Wananchi sasa wameshuhudia kodi zao zikigeuka barabara na madaraja yanayorahisisha maisha yao ya kila siku, huku wachimbaji wa dhahabu wa Nyakafuru wakisisitiza kuwa barabara hii ni ushindi wa vitendo, unaowafanya kutokubali tena maneno ya wapinzani.

 


Post a Comment

0 Comments