TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

MWENGE WA UHURU WAPONGEZA TARURA GEITA: MIRADI MITATU YAUNGURUMA KWA UBORA


Na Victor Bariety, Geita;

Septemba 2025


Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025 umeendelea kutoa heshima kubwa kwa Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) mkoa wa Geita, baada ya kuzindua rasmi mradi wa boksi kalavati katika barabara ya Kharumwa–Nyijundu, wilayani Nyang’wale.

 


Uzinduzi huo umeweka historia, kwani ni mara ya tatu mfululizo ndani ya wiki moja miradi ya TARURA Geita kuibua pongezi kutoka kwa kiongozi wa mbio hizo, Ndg. Ismail Ali Ussi. Awali Mwenge huo ulipita na kuridhishwa na miradi ya barabara ya Nzera (Wilaya ya Geita) na Kasco (Manispaa ya Geita), na sasa umehitimisha na mradi wa Nyang’wale.

 

Pongezi kutoka kwa kiongozi wa Mwenge

Akitoa kauli yake baada ya ukaguzi, Ndg. Ussi alisisitiza kuwa Geita imeonesha mfano wa kuigwa kitaifa.

 “Nimepitia miradi hii kwa makini, nimeona nyaraka na kazi iliyofanyika. Hakuna dosari. Hii ndiyo inayoonesha fedha za wananchi zinatumika ipasavyo. Hongereni sana TARURA,” amesema na kisha kutangaza uzinduzi rasmi wa mradi huo.

 


Maelezo ya kitaalamu

Kwa mujibu wa Meneja wa TARURA Wilaya ya Nyang’wale, Mhandisi John Msita, mradi huo uligharimu shilingi 579,680,000.00, ukifadhiliwa na Benki ya Dunia kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

 


Kazi zilizotekelezwa zilihusisha ujenzi wa boksi kalavati mbili za zege, kalavati ndogo nane, pamoja na matengenezo ya kilomita moja ya barabara ya changarawe. Kazi ilianza Juni 18, 2024 na kukamilika Aprili 14, 2025 na ilifanywa na kampuni ya D4N Company Ltd kutoka Kahama.

 


Mhandisi Msita aliongeza kuwa mradi huo umeondoa usumbufu mkubwa uliokuwa ukiwalazimisha wananchi kuzunguka umbali wa kilomita 98 kufika makao makuu ya Wilaya ya Nyang’wale, Kharumwa. Kwa sasa umbali huo umepungua na kufikia kilomita 90 pekee.

 


Manufaa kwa wananchi

Wananchi wa Kijiji cha Bukungu, wakiongozwa na mwenyekiti wao Hadija Samson, walieleza jinsi walivyokuwa wakiteseka kabla ya mradi huo.“Zamani tulivuka kwenye daraja la miti, tena kwa kulipia ada ya shilingi 500 kwa miguu na shilingi 5,000 kwa pikipiki. Wengi walihatarisha maisha yao wakati wa mafuriko. Lakini leo tuna daraja imara la zege. Tunamshukuru Rais Samia, TARURA na viongozi wetu wa CCM kwa kazi kubwa,” amesema Hadija huku akishangiliwa.

Ujumbe wa amani na maendeleo

Zaidi ya kuzungumzia mradi huo, Ndg. Ussi alitumia nafasi hiyo kuwakumbusha wananchi juu ya amani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

 “Kumchagua Rais Samia ni kuchagua maendeleo—barabara, madaraja, maji, umeme na afya. Lazima tulinde amani ili vizazi vijavyo vibaki na miradi hii,” amesitiza.

 


Geita yaandika ukurasa mpya

Kwa mara ya kwanza, miradi mitatu mfululizo ya TARURA katika mkoa mmoja imepata sifa ya kiwango cha juu mbele ya Mwenge wa Uhuru. Hali hii imeweka rekodi mpya Geita, tofauti na hali ya miaka ya nyuma katika maeneo mbalimbali nchini ambapo baadhi ya miradi haikuzinduliwa kwa kuwa haikukidhi viwango.

 


Wananchi sasa wanaona ushahidi wa kodi zao zikigeuka miundombinu ya maana, ikirahisisha biashara, usafirishaji na maisha ya kila siku. TARURA Geita imejipambanua kama kielelezo cha uwajibikaji na nidhamu katika utekelezaji wa miradi ya barabara nchini.

 


Hata hivyo, Mwenge wa Uhuru Kitaifa 2025 bado unaendelea mkoani Geita ukizindua miradi mbalimbali ya maendeleo iliyo chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan. Hadi sasa, hakuna mradi uliokosolewa kwa kujengwa chini ya kiwango, lakini pale unapoifikia miradi ya TARURA, mkimbiza Mwenge amekuwa akimwaga sifa nyingi zaidi. Hali hiyo imeongeza morali na uadilifu kwa watumishi wa TARURA kuona mchango wao katika taifa unatambulika, kana kwamba ni tuzo ya kufanya vizuri.

 


Licha ya kuwepo miradi ya sekta nyingine kama afya na maji, miradi ya TARURA imekuwa kivutio kikubwa kwa kiongozi wa Mwenge. Leo Mwenge unaendelea kukimbizwa katika Wilaya ya Mbogwe ukizindua miradi mbalimbali, na kwa kuwa TARURA tayari wameanza vizuri, wafanyakazi wake wanaamini hata miradi iliyopo Mbogwe, Bukombe na Chato nayo itafunika kwa ubora. Hayo ni kwa mujibu wa Meneja wa TARURA Mkoa wa Geita, Mhandisi David Msechu.

 

PICHA ZAIDI.







Post a Comment

0 Comments