TANGAZA NASI: geitapressclub@gmail.com

NEEC YAINUFAISHA KIGOMA

Katibu Mtendaji wa Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) CPA Beng'I Issa

Na Urban Epimark, KIGOMA

Maonesho ya Sita ya Mifuko ya Program za Uwezeshaji hapa nchini yanayo ratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) yanayo endelea katika mji wa Kigoma katika viwanja vya Mwanga Community Centre yamekuwa ya manufaa makubwa kwa wakazi wa Kigoma wakiwemo wajasiriamali na wafanyabiashara. 

Maonesho hayo yaliyo anza Mei 21, 2023 yanatarajiwa kufikia tamati siku ya Jumamosi Mei 27, 2023  na Mgeni Rasmi siku hiyo ni Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Kassim Majaliwa, huku yakiongozwa na Kaulimbiu "kutumia mabadiliko ya kidigitali katika mifuko ya uwezeshaji pamoja na program zake"

Mkurugenzi wa Uwezeshaji na Ushiriki wa Watanzania kutoka Ofisi ya Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) Makao makuu Dodoma, Bi Neema Mwakatobe amewaeleza waandishi wa habari kwenye maonesho hayo kwamba, idadi kubwa ya wakazi wa mkoa wa Kigoma na mikoa ya jirani wakiwemo wajasiriamali na wafanyabiashara zaidi ya sabini (70) wamefanikiwa kupatiwa mafunzo ya Uwezeshaji kutoka kwa taasisi mbalimnali zilizo andaliwa kufundisha madarasa ya wajasiriamali kwenye maonesho hayo.

Lengo la maonesho hayo ni kutoa fursa kwa umma wa mkoa wa Kigoma pamoja na mikoa ya jirani kupata elimu mbalimbali kutoka kwa taasisi zinazo jishughulisha na urasmishaji biashara za wananchi ili  kuwapatia elimu ya jinsi ya kunufaika na program za mifuko mbalimbali ambayo ni sabini na mbili (72) iliyopo  chini ya uratibu wa Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ili wananchi waijue na kuitumia kuendeleza biashara zao na kusaidia kutoa ajira na kuondoa umaskini nchini.

Afisa wa NEEC anae shughulikia masuala ya "Local Content" Bi Suzan Massala (kushoto) akimwelezea kwenye maonesho ya 6 ya mifuko ya Uwezeshaji yanayoendelea mjini Kigoma Mhadhiri wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) Dkt Hussein Nzao (kulia) jinsi NEEC inavyo wawezesha wananchi kuwa na viwango vya kimataifa vya kuhudumia miradi ya kimkakati hapa nchini.

Mbali na madarasa ya mafunzo kwenye maonesho hayo ambapo palitengwa wasaa wa kutosha kwa taasisi mbalimbali kutoa mafunzo, NEEC iliandaa pia meza maalum kwa kila taasisi kwenye maeneo ya viwanja vya maonesho kukutana na wanao fika kwenye hayo maonesho  ili kupatiwa ufafanuzi wa mambo kadhaa wa kadhaa.

Kwenye banda la NEEC, Afisa Uwezeshaji Mwandamizi anae shughulikia masuala ya ushiriki wa watanzania kwenye miradi ya kimkakati (Local Contents) Bi Sizan Massala alitoa maelezo ya ufafanuzi kwa watu wa kada mbalimbali waliofika kwenye meza ya NEEC kuhusu Baraza linavyo wezesha kampuni za kitanzania kukua kiuzalishaji na pia kuwa na vigezo vya kutoa huduma na uuzaji wa bidhaa kwenye miradi mikubwa inayo jengwa nchini pamoja na maeneo ya  wawekezaji kutoka nje ya Tanzania.

Moja ya Mafanikio makubwa ya Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi anaeleza Afisa Uwezeshaji wa NEEC Bw Omar Haji kutoka Kitengo cha Uratibu wa Mifuko na program za uwezeshaji kwamba ni kuanzishwa kwa mpango wa  uchumi wa viwanda unaoitwa SANVN VIWANDA SCHEME.

Baadhi ya matokeo ya kujivunia ya Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) ni kupitia mpango wa uwezeshaji wa SANVN VIWANDA SCHEME ambao unatekekezwa kwa pamoja baina NEEC na taasisi zingine Nne za SIDO, Azania Bank, NSSF na VETA. Katika picha ni Meneja Mauzo wa kampuni ya kitanzania ya B & L Agri-Digital Bw Frank Kilongola (kushoto) ambayo iliwezeshwa kupata mtaji wa kujiendesha (working capital) na kuweza kutengeza mafuta ya Alizeti kwa kiwango cha kimataifa na kufungasha kwenye vifungashio vyenye ubora wa kukidhi mahitaji ya mnunuzi kufuatana uwezo wake kifedha.

Mpango huu unatoa mikopo kwa wenye viwanda wajasiriamali wadogo kuanzia milioni 8 hadi milioni 50, wajasiriamali wa kati ni milioni 50 hadi milioni 500.

"Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) linajivunia kuanzishwa kwa mpango wa SANVN VIWANDA SCHEME kwa kushirikiana na taasisi tano za NEEC, SIDO, VETA, NSSF na Benki ya Azania" anaeleza Afisa Uwezeshaji Bw Omar Haji.

Bw Haji anaendelea kuelezea mafanikio katika mpango wa viwanda scheme ya kwamba, kampuni za kitanzania nyingi zimeanzishwa na kuwezesha kutoa ajira nyingi pamoja na kuchangia patoa serikalini na kupunguza umaskini kupitia  Baraza la Uwezeshaji kwa  kuwezeshwa mikopo ya uwekezaji (investment loans) na mikopo ya uendeshaji kampuni hizo yaani working capitals.

Katika maandalizi ya kufanyika maonesho ya 6 ya program ya mifuko ya uwezeshaji, Katibu Mtendaji wa NEEC CPA Beng'I Issa (wa pili kutoka kulia) pamoja na wasaidizi wake walifanya vikao mbalimbali kuwashirikisha wakuu wa taasisi kuwakaribisha kushiriki kutoa elimu kwenye maonesho hayo. Katika picha Katibu Mtendaji akiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi ya Mamlaka ya Elimu yaani TEA Bi Bahati Geuzye (wa pili kutoka kushoto). Mwingine kushoto ni Mkurugenzi wa Uwezeshaji na Ushiriki wa Watanzania kutoka NEEC Bi Neema Mwakatobe (blaus nyekundu) na mwanzo kulia ni Afisa Uwezeshaji wa NEEC Bw Omar Haji kutoka kitengo cha Uratibu wa Mifuko na program za uwezeshaji.

Mifano halisi ya wanufaika wa mpango wa SANVN VIWANDA SCHEME ni kampuni ya B & L Agri-Digital  ya jijini Dar es Salaam iliyo wezeshwa mtaji wa kujiendesha (working capital) ambapo kampuni hiyo kwa sasa ina zalisha mafuta ya Alizeti ya chapa au brand ya San Rich yenye ubora wa kimataifa (triple refinary edible oil)  na kuyafungasha kwenye vifungashio sahihi vyenye kuhimili ushindani sokoni lakini pia katika ujazo wa hali zote (mdogo, kati na mkubwa) na kuwezesha mwenye kipato kidogo na kikubwa kununua.

Kampuni hiyo iliyo anzishwa nchini mwaka 2019 ambayo ilianza kwa kufanya utafiti kuhusu changamoto za upatikanaji mafuta ya kupikia, imewezesha kutoa ajira kwa vijana wa kitanzania jijini Dar es Salaam na Dodoma zaidi ya 50 na pia inachangia pato serikalini kwa kulipa kodi na kwa sasa inauza bidhaa zake nyingi katika mikoa ya kusini ya Lindi, Mtwara, Songea lakini pia Morogoro, Pwani na Kahama.

Meneja wa Mauzo wa B & L Agri-Digital Bw Frank Kilongola anaeleza zaidi kwamba, kampuni hiyo inalenga miaka ya usoni  kuuza bidhaa zake nje ya nchi hususani kwenye maduka makubwa (Supermarkets) kwani wanavyo vigezo vyote vya kuuza nje ya mipaka ya Tanzania ikiwemo Barcodes kutoka GS1-Tanzania.

Timu ya waratibu inayo shirikisha wajumbe kutoka NEEC, SIDO, VETA, NSSF na Benki ya Azania kwenye ziara ya kutembelea wanufaika na wahitaji wa mkopo wa SANVN Viwanda Scheme wakiwa katika picha ya pamoja. NEEC ndie mratibu wa mpango ambapo maombi hupokelewa ofisi za SIDO au VETA kisha, benki ya Azania hufanya uhakiki wa mwombaji endapo ana vigezo vya kukopeshwa na mpango, kisha mfuko wa NSSF kwa niaba ya serikali hutoa fedha za kumwezeshaji mwombaji kupitia benki ya Azania.

Mnufaika mwingine wa mpango wa SANVN VIWANDA SCHEME ni kampuni iliyoanzishwa na kuongozwa na mwanamama wa kitanzania Bi Violet Oscar pia kutoka mkoani Dar EsSalaam anae miliki kampuni ya kutengeneza vijiti vya meno (toothpicks) na vibaniko vya nyama (bamboo skewers) 

Watanzania wengi wanakumbuka jinsi wabunge wetu walivyo kuwa siku za nyuma wakilalamikia uagizaji wa vijiti vya meno, sindano na hata nyembe kutoka nje, ambapo kampuni za kitanzania hazikuwa kutengeneza bidhaa hizi nchini.

Lakini kwa kupitia Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) chini ya mpango wa SANVN VIWANDA SCHEME mtanzania huyu mwanamke amewezeshwa mtaji na sasa ameondoa pengo la Tanzania kuagiza vijiti vya meno kutoka China.

Afisa Mtendaji Mkuu wa GS1-Tanzania Bi Fatuma Kange (pichani) ambae taasisi yake inasaidia kutoka Msimbomilia au Barcodes kwa bidhaa zote zinazo zalishwa nchini. Tanzania ilipata ithibati ya Barcodes kutoka GS1 Global yenye makao makuu yake mjini Brusels nchini Ubelgiji tangu November 2011 baada ya serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara kutoa kibali rasmi na kuwezesha kupatiwa kiambishi cha utambuzi wa bidhaa kiulimwengu kwa Tanzania ambacho ni namba #620. Barcodes za GS1-Tanzania zinatambulika na kutumika mataifa 118 ulimwenguni. Hivyo basi kuanzia mwaka 2011, bidhaa za Tanzania zinazo zalishwa na wajasiriamali na wenye viwanda zaidi ya 5000 nchini tayari zimepatiwa Barcodes kutoka GS1-Tanzania na kuwa kiungo muhimu sana cha mafanikio ya Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) katika kufikia malengo yake.

"Nina shukuru Baraza la Uwezeshaji (NEEC) kunishika mkono kuniwezesha hadi nimeanzisha na kumiliki kampuni yangu ya Bongo Toothpicks Industry na sasa nimeweza kutoa ajira kwa watanzania zaidi ya hamsini (50)  na pia kulipa kodi serikalini na pia kuwezesha bidhii hizi kupatikana nchini" anaeleza Bi Violet Oscar Mkurugenzi wa Bongo Toothpicks Industry.

Bi Violet Oscar anaeleza historia yake kwamba alikuwa mwajiriwa katika taasisi fulani hapa nchini. Hakuridhika na maisha ya kuajiriwa. Kipindi hicho ndipo Tanzania ilikuwa ikihimiza sera ya Tanzania ya Viwanda  na ndipo yeye akaiona fursa ya kutengeneza vijiti vya meno na kujifunza ujuzi wa kuvitengeneza kwa njia ya kusoma mtandaoni. Huu ni ujasiri mkubwa sana kwa mwanamke wa kitanzania.

Alimpata mtaalam kutoka nchini China ambae walikuwa wakiwasiliana kwa mtandao lakini bila wao kujuana uso kwa uso. Raia huyu wa China alimfundisha na kumwelekeza kwa njia ya mtandao na pia kumtumia aina ya mashine ya kutengeza bidhaa hiyo.

Shirika la kuendeleza viwanda vidogo nchini yaani SIDO kwa muda wote imekuwa kiungo kikubwa katika mpango wa SANVN VIWANDA SCHEME. Katika picha ni Meneja wa Huduma za Kifedha kutoka SIDO Makao Makuu DSM Bi Jacqueline Misawala ambae amesema katika maonesho hayo ya mifuko ya program za uwezeshaji kwamba yamekuwa ya Baraka kubwa kwa waandaaji na wananchi wa Kigoma, kwani wamepata fursa za mafunzo na pia kuuliza ufafanuzi wa jinsi ya kusaidiwa na mifuko hiyo ya uwezeshaji ili kuendelea kujikwamua kiuchumi.

Bi Violet Oscar kipindi hicho alikuwa akizalisha kwa kutumia mianzi ya kienyeji (Local bamboo trees) na eneo lake la uzalishaji lilikuwa Bunju, Dar es Salaam. 

Aliamu kujiendeleza kwa kupata mafunzo zaidi SIDO na baadae kuomba mkopo kupitia SANVN VIWANDA SCHEME na kuwezeshwa mtaji wa kupanua uzalishaji wake. Alipewa mkopo wa kununua mashine na vipuli vya kutosha na kuhamishia kiwanda chake wilayani Kisarawe mkoani Pwani na kwa sasa ameajiri watanzania zaidi ya hamsini (50) na analipa kodi serikalini, huku akisema anaona mafanikio makubwa siku za usoni kibiashara. 

Changamoto anazo kutana nazo Bi Violet Oscar katika uzalishaji wake lakini pia kwa upande wa pili ni fursa kubwa kwa wakulima, ni uhaba wa miti ya kisasa ya mianzi kwa ajili ya kuzalishia vijiti vya meno na vibaniko vya nyama.

Mmoja wa wajasiriamali kutoka mkoani Dar es Salaam aliyeshiriki maonesho hayo mkoani Kigoma Bi Ester Mhanga ambae ni mmiliki wa kampuni ya Mhambe Edeni Products inayo tengeneza Unga Lishe kwa kutumia maharagwe ya Soya, ameipongeza serikali kupitia Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) kwa kuwajali wajasiriamali wa chini, ikiwa yeye aliwezeshwa mtaji wa kiasi cha Milioni 15, kupitia mpango wa mapato ya asilimia 10% kutoka Manispaa ya Kinondoni mkoani Dar EsSalaam.

"Nimeshaenda kuonana na Wakala wa usimamizi na uendelezaji  misitu hapa nchini yaani TFS na kuwaelezea changamoto yangu kuhusu ukosefu wa miti ya kisasa ya mianzi na wao wameshanielewa. TFS wamesha anzisha vitalu vya miti ya mianzi ya kisasa (hybrid bamboo trees) na kwa sasa wana karibia kuvuna" anaeleza Bi Violet Oscar.

Katika kuhitisha makala hii, zipo shuhuda nyingi kwa Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) kwa manufaa ya watu wa Kigoma kupitia maonesho haya ya Sita (06) ya mifuko ya uwezeshaji na program zake hapa nchini.

Wito umeendelea kutolewa kwenye maonesho hayo kwamba, wananchi wa mjini Kigoma na maeneo ya jirani waendelee kufika  kutembelea maonesho hayo kwani bado muda upo, ili wajifunze kwa hawa wachache wenye shuhuda za mafanikio ya Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi yaani NEEC. 


Mwisho.

Post a Comment

0 Comments